Tuesday, 7 April 2020

JIANDAYE KUTOA HESABU


 SIKU YA HUKUMU, KILA MMOJA ATATOA HESABU YA UTUMISHI WAKE.
(Each of us will give an account of oneself on the Day of Judgment)

“Iangalie sana huduma ile uliyopewa katika Bwana, ili uitimize. (Wakolosai 4:17).

Huduma katika kanisa la Mungu ni kazi ya kila kiungo. Japo vipo viungo vilivyopewa heshima zaidi ya vingine. Paulo anasema, “Basi katika nyumba kubwa havimo vyombo vya dhahabu na fedha tu, bali na vya mti, na vya udongo; vingine vina heshima, vingine havina.” (2 Timotheo 2:20) Vyombo vyote hivi havikujileta vyenyewe ndani, vililetwa na mwenye nyumba akiwa na kusudi kwa kila kimoja. Vya dhahabu japo ni vya thamani zaidi ya vingine havitatumika maeneo yote; kuna maeneo tunahitaji vya udongo, kwingine vya mti au vya fedha. Mwenye nyumba ndiye anayejua thamani na matumizi ya kila kimoja.

Ndivyo ilivyo kwa kanisa la Mungu; kila aliyeokoka ni chombo na ameitwa kwa jinsi yake. Anaweza akawa chombo cha dhahabu (wenye karama na vipawa zaidi), au cha fedha (Wenye wito Fulani), au cha mti au cha udongo (washirika na wenye karama zinazoonekana kibinaadamu kwamba hazina thamani). Sijui mimi na wewe ni vyombo vya aina gani, ila ninachojua ni kwamba sote tu vyombo vya Bwana. Katika kitabu cha Warumi 4:08 Paulo anatueleza juu ya kitu alichokifanya Yesu alipoinuliwa: anasema, “Alipopaa juu aliteka mateka, Akawapa wanadamu vipawa.” Kisha akavitaja: “Naye alitoa wengine kuwa mitume, na wengine kuwa manabii; na wengine kuwa wainjilisti na wengine kuwa wachungaji na waalimu; kwa kusudi la kuwakamilisha watakatifu, hata kazi ya huduma itendeke, hata mwili wa Kristo ujengwe”

Hapa neno linatuweka wazi kwamba kusudi la Mungu kuwapa watu vipawa ni ‘kazi ya huduma itendeke na mwili wa Kristo (kanisa) ujengwe” Hili ndilo lengo kuu, hivyo mtumishi yeyote anayefanya kinyume na hayo ni mharibifu. Kama amekuwa kwazo kwenye kazi ya huduma au anaubomoa mwili wa Kristo (kanisa) huyo ni mchungaji au mtumishi aliyepoteza sifa kabisa. Sifa mojawapo ya mtumishi ni kuwa mtendakazi mwenye uchungu na kondoo (kazi). Ni lazima aone wale kondoo (watu) anaowatumikia kama mali yake (japo si mali yake). Awapende na awatumikie kwa upendo.

Warumi 12:4-14
Kwa kuwa kama vile katika mwili mmoja tuna viungo vingi, wala viungo vyote havitendi kazi moja; Vivyo hivyo na sisi tulio wengi tu mwili mmoja katika Kristo, na viungo, kila mmoja kwa mwenzake. Basi kwa kuwa tuna karama zilizo mbalimbali, kwa kadiri ya neema mliyopewa; ikiwa unabii, tutoe unabii kwa kadiri ya imani; ikiwa huduma, tuwemo katika huduma yetu; mwenye kufundisha, katika kufundisha kwake; mwenye kuonya, katika kuonya kwake; mwenye kukirimu, kwa moyo mweupe; mwenye kusimamia kwa bidii mwenye kurehemu, kwa furaha. Pendo na lisiwe na unafiki lichukieni lililo ovu, mkiambatana na lililo jema. Kwa pendo la udugu, mpendane ninyi kwa ninyi; kwa heshima mkiwatanguliza wenzenu; kwa bidii, si walegevu; mkiwa na juhudi katika roho zenu; mkimtumikia Bwana; kwa tumaini, mkifurahi; katika dhiki, mkisubiri; katika kusali, mkidumu; kwa mahitaji ya watakatifu, mkifuata ukarimu; katika kukaribisha wageni mkijitahidi. Wabarikini wanaowaudhi; barikini, wala msilaani.

Mistari hii inatuweka wazi zaidi juu ya utofauti wetu katika kazi ya Mungu na jinsi ambayo tunaweza kuzitumia tofauti hizo kutumikiana kwa utukufu wa Mungu. Paulo anasema ‘sisi ni kama viungo katika mwili’ na tunapaswa kufanya kazi katika pendo lisilo na unafiki, tena kwa bidii tukiwatanguliza wengine. Mtumishi wa Mungu anapokwenda kinyume na kanuni hizi alizoziweka Mungu, moja kwa moja anakuwa mharibifu. Ona Paulo anavyosema tena: “ili kusiwe na faraka katika mwili, bali viungo vitunzane kila kiungo na mwenziwe.” (1 Wakorintho 12:25)

Kila mtumishi aliyeitwa na Mungu haijalishi ni mtume au nabii au mchungaji au mwinjilisti au mwimbaji au mwingine yeyote, ni kiungo kimoja katika mwili wenye viungo vingi. Ni chombo miongoni mwa vyombo vingine. Ni (mtumishi) mtumwa wa Kristo miongoni mwa watumishi wengine. Paulo anasema tena, “Basi uvueni uongo, mkaseme kweli kila mtu na jirani yake; kwa maana tu viungo, kila mmoja kiungo cha wenzake. (Waefeso 4:25). Kwa hiyo hakuna jinsi ambavyo mtumishi awaye yote anaweza kudai kwamba yeye yuko juu ya wengine au mkuu kuliko wengine; akifanya hivyo anakuwa mharibifu.

Kwa utangulizi huu mfupi nasimama kwa ujasiri wote kukuambia wewe mtumishi mharibifu: Ole wako, tena narudia Ole wako, usipotubu na kugeuka Ole wako. Yeremia alitabiri akasema, “Ole wao wachungaji, wanaoharibu kondoo za malisho yangu na kuwatawanya! Asema Bwana.” (Yeremia 23:1) Hapa Mungu alikuwa anazungumza juu ya watu wake Israeli. Na mimi juu ya kanisa la Kristo niseme, “Ole wako mchungaji au mtumishi yeyote unayewaharibu kondoo wa malisho ya Mungu (kanisa) na kuwatawanya! Utakuja kutoa hesabu. Usijitie moyo kama sifa unazopewa na watu, usifurahie kusanyiko kubwa linalokujia, usiangalie hiyo fedha ya aibu unayojikusanyia ukajiona mjanja! Kiburi chako kitashushwa hakika! Hata ukiharibu sasa, hautaharibu milele. Geukaaa!
  •           Wewe unayefundisha mafundisho ya uongo ili kujikusanyia watu kwa hila: Ole wako!
  •       Wewe unayeshika mapokeo ya dini na kuikataa kweli ya Mungu: Ole wako!
  • -          Wewe unayejiita nabii wa Mungu huku ukijua kuwa wewe ni mchawi na mshirikina: Ole wako!
  • -          Wewe unayewadanganya watu wa Mungu na kujikusanyia fedha ili kujishibisha mwenywe badala ya kuujenga mwili wa Kristo: Ole wako!
  • -          Wewe uliyegeuza nyumba ya Mungu kuwa pango la wanyang’anyi kwa kuuza kipawa cha Mungu: Ole wako!
  • -          Wewe unayefanya mzaha na kazi ya Mungu, na kuwavunja wengine moyo, na umeshupaza shingo ukijifaanya husikii maonyo: Ole wako!
  • -          Wewe uliyejiinua juu na kujipa utukufu mwenyewe, ukilitangaza jina lako kuliko jina la Yesu: Ole wako! Mungu atakapokuangusha, hutainuka tena.
  • -          Wewe unayelichezea Neno la Mungu, kwa kulichanganya na uongo, ukiwafurahisha watu kwa unafiki, utaunywa uchungu wa unafiki wako: Ole wako!
  • -          Wewe unayejiita Mkuu, na kujipa majina makubwa, huku ukiwanyanyasa watu, na kuwalaghai, kazi yako inanuka mbele za Mungu, hutafika mbali: Ole wako usipogeuka na kutubu.
  • -          Wewe unayejisumbukia huku ukivutwa na tamaa ya mali, tamaa ya mwili na kiburi cha uzima, na kusahau wito ulioitiwa, mali zimekuwa Mungu wako, umekataa kumtii Mungu kwa sababu ya tumbo: Ole wako!
  • -          Yesu anasema, “Hakuja kuleta amani duniani, alikuja kuleta upanga! Wewe nabii unapata wapi amani ya kujistarehesha na anasa, kula na makahaba na wazinzi, umepata wapi nafasi hiyo! Ole wako!
  • -          Ole wako unayelinajisi kanisa la Mungu kwa uzinzi na uasherati, jina lako linanuka mbele za Mungu. Unazini na wale unaowatumikia, Ole wako!
  • -          Ole wako mchungaji mvivu na mzembe, unaowaacha kondoo wakitaabika; na wewe unazurura mitaani kutafuta mali, hakika utatoa hesabu.
  • -          Kazi ya Mungu inafanyika kwa mazoea, mizaha imepanda mpaka madhabahuni, uhuni umejaa, ukahaba umelitawala kanisa na wachungaji mmenyamaza: Ole wenu!
  • -          Heri yao waliokubali kuonekana wabaya, wakapiga kelele juu ya ukahaba! Kanisa la Mungu limechubuka, linavuja damu. Wachungaji wanachekelea mapato, na kujenga majumba makubwa! Huu ni msiba, manabii wa kweli mko wapii? Mitume mko wapi? Waalimu mbona mmenyamaza? Wainjilisti hamwoni shetani akikokota roho za watu Jehanamu? Waimbaji mnaimba nini? Ni nani aliyewaita? Baba yenu ni nani?
  • -          Heri yako wewe ulichagua kufa kwa ajili ya Haki, heri yako uliyeamua kubaki maskini wa mali huku ukiihubiri kweli ukimngoja Mungu akukweze kwa wakati wake. Ujapokuwa maskini, unawatajirisha wengi katika ufalme wa Mungu.
  • -          Heri yako unayelia juu ya uharibifu unaoendelea juu ya dunia; heri yako ambaye moyo wako umeja huruma unapowatazama wajane, mayatima, maskini, wenye njaa, omba omba barabarani, wakimbizi, wafungwa, wagonjwa na wanaoteseka katika dhambi; Mungu wetu ni mwenye huruma, hakika atakukumuka.

Huu si wakati wa kutafuta umaarufu, si wakati wa kufanya maigizo madhabahuni, si wakati wa kutafuta vyeo, si wakati wa kung’ang’ania madhehebu, si wakati wa kupasuka pasuka na kujitenga na wengine, si wakati wa kuoneana wivu, si wakati wa kugombana watumishi, si wakati wa kujiona bora kuliko wengine; ni wakati wa kudhihirisha kufa kwetu pamoja na Kristo, ni wakati wa kuyatafuta mapenzi ya Mungu na kuyatenda. Yesu yu karibu kurudi kulichukua kanisa lake. Ni wakati wa kuliandaa kanisa kwa ajili ya unyakuo.

Ni nyakati za mitume kusimama kama mitume katika mapenzi ya MUNGU, manabii kusimama kama manabii katika mapenzi ya Mungu, na wachungaji nao vivyo hivyo, wainjilisti, waalimu, viongozi, waimbaji nawengine wote vivyo hivyo. Kanisa si majengo, ni kusanyiko la watu waliotengwa kwa ajili ya kusudi la Mungu. Wewe unayeng’ang’ania kumiliki kanisa mwenyewe, pole! Wewe unayeng’ang’ania dhehebu linalomkataa Yesu na kufundisha uongo, pole: Wewe ni mtumishi wa shetani, na shetani ndiye baba yako. Huwezi kuwa mtumishi wa Mungu huku wewe ni mlevi, mzinzi, mwalimu wa uongo, mnafiki, msengenyaji, mla rushwa, mkatili, na mengine kama hayo; hakika huwezi.
          Nabii Ezekieli aliambiwa atoe unabii juu ya Wachungaji (viongozi, watumishi) wa watu wa Mungu Israeli. Neno linasema, “Mwanadamu, toa unabii juu ya wachungaji wa Israeli, toa unabii, uwaambie, naam, hao wachungaji, Bwana MUNGU asema hivi; Ole wao wachungaji wa Israeli, wanaojilisha wenyewe; je! Haiwapasi wachungaji kuwalisha kondoo?” Jambo hili ni jambo la kusikitisha sana; yaani wachungaji kujilisha wenyewe na kusahau kulisha kondoo. Ubinafsi wa namna hii ndio uliolivamia kanisa la nyakati za leo, hasa kanisa lililo Afrika. Matumbo yetu yamekuwa makubwa kiasi cha kutupofusha tusione mateso ya kondoo tuliopewa kuwachunga. Mahitaji yetu yametufanya viziwi tusiweze kusikia vilio vya kondoo wanaotaabika katika nyika wasione wa kuwapa hata tone la maji.

            Paulo akiwa katika Roho Mtakatifu, aliongea katika hali ya huzuni kubwa juu ya watu wanaohubiri Injili ya namna nyingine na kuipotosha kweli ya Mungu. Alisema, “Lakini ijapokuwa sisi au malaika wa mbinguni atawahubiri ninyi injili yo yote isipokuwa hiyo tuliyowahubiri, na alaaniwe.” Tena akarudia kwa mkazo zaidi akasema, “Kama tulivyotangulia kusema, na sasa, nasema tena, mtu awaye yote akiwahubiri ninyi injili yo yote isipokuwa hiyo mliyoipokea, na alaaniwe.” (Wagalatia 1:8-9) Wewe nabii na mwalimu wa uongo, laana hii huwezi kuiepuka! Labda uamue leo kutubu na kuamua kuihubiri iliyo Kweli. Ninajua nafsi yako inakushuhudia kitu juu ya hayo unayofundisha. Wewe unayefundisha ili upate mali na kulishibisha tumbo, ole wako.

            Ujumbe huu umekujia ili usiwe na la kujitetea mbele za Mungu. Biblia unayoichezea kwa kuitafsiri kama unavyotaka au kwa kusukumwa na Ibilisi uliyeamua kumtumikia, iliandikwa kwa machozi na damu. Mitume walikubali kuteswa hata kuuawa wakiitetea Imani ya kweli. Leo hii unasimama, unajiita nabii, mtume, mwalimu au hata mchungaji, kumbe ni mwigizaji, mlaghai na mjumbe wa shetani; hakika hutafika mbali. Jiulize leo umeua wangapi na uongo uliofundisha! Angalia vilio ulivyosababisha kwa sababu ya tamaa yako ya fedha. Watu wanakufa kwenye dhambi, huku ukujitajirisha na kuona fahari. Unatabiri uongo hata wewe mwenyewe unajua! Saa yaja na sasa ipo, utakaposimama mbele ya kiti cha hukumu kutoa hesabu mbele za Mungu. Sijui utajibu nini!

            Mtume Yakobo anaonya na kusema, “Ndugu zangu, msiwe waalimu wengi, mkijua ya kuwa mtapata hukumu kubwa zaidi.” (Yakobo 3:1) Leo kila mtu anajiita nabii, mwalimu, mchungaji, mtume na mengine, wakifikiri ni sifa. Kumbe ni msalaba, huduma si ufahari. Huduma ni msalaba, ni kushiriki mateso pamoja na Kristo. Ufahari wetu u katika Kristo. Tukiishi tunaishi pamoja naye, tukifa tunakufa pamoja naye, tukiudhiwa tunaudhiwa pamoja naye, tukitukanwa na kukakataliwa tunakuwa pamoja naye! Hii ndiyo fahari tuliyonayo. Magari, majumba, fedha na vyote vya ulimwengu huu ni ziada kwetu. Ufalme wa Mungu ndio kipaumbele chetu.
          Mwisho niseme, “Watumishi wenzangu, “tukiwa tumefufuliwa pamoja na Kristo tuyatafute yaliyo juu Kristo aliko, ameketi mkono wa kuume wa Mungu. Tusikubali kuwa na majina ya kuwa hai kumbe tumekufa, tung’ang’anie uhai wetu katika Kristo. Tuwe watu wa kujichunguza kila siku tukijikumbusha kama Paulo alivyojisema, “bali nautesa mwili wangu na kuutumikisha; isiwe, nikiisha kuwahubiri wengine, mwenyewe niwe mtu wa kukataliwa.” (1Wakorintho 9:27) Tena tukatae kulichanganya Neno la Mungu nauongo. Tusiwe watu wa kupenda fedha ya aibu, tutumike kwa uaminifu hata kufa. Tuungane na mtume Paulo tena katika maneno haya:
 “Kwa sababu hiyo, kwa kuwa tuna huduma hii, kwa jinsi tulivyopata rehema, hatulegei; lakini tumekataa mambo ya aibu yaliyositirika, wala hatuenendi kwa hila, wala kulichanganya neno la Mungu na uongo; bali kwa kuidhihirisha iliyo kweli twajionyesha kuwa na haki, dhamiri za watu zikitushuhudia mbele za Mungu.” (2 Wakorintho 4:1-3)

            Neno linasema,Na Mchungaji mkuu atakapodhihirishwa, mtaipokea taji ya utukufu, ile isiyokauka. (1 Petro 5:4) Naye Mungu antayafuta machozi yetu tukishaondoka katika ulimwengu huu. Tusikubali kubaki na miujiza, kunena kwa lugha na matendo ya Imani huku tukiwa hatuna upendo wa kweli na Mungu. Yesu anasema, “Wengi wataniambia siku ile, Bwana, Bwana, hatukufanya unabii kwa jina lako, na kwa jina lako kutoa pepo, na kwa jina lako kufanya miujiza mingi? Ndipo nitawaambia dhahiri, Sikuwajua ninyi kamwe; ondokeni kwangu, ninyi mtendao maovu. Usijitie moyo na miujiza, angalia mahusiano yako na Mungu zaidi ya miujiza. Angalia usije ukapata hasara ya nafsi yako! Utumishi si tiketi ya kuingia mbinguni. Ni lazima tuwe watakatifu.

Ifike mahali kuishi kwetu kuwe ni Kristo. Na tuwe watakatifu kama Mungu wetu alivyo mtakatifu. Tusitumike kwa hila, bali kwa adili tukimzalia Mungu matunda kwa utumishi uliotumika. Tusiwe kwazo la namna yoyote ili utumishi wetu usilaumiwe, bali kwa kila jambo tujipatie sifa njema (2Wakorintho 6:3-4). Tukubali kuwa Nuru ing’aayo gizani, tukikataa kila lililo baya. Tusiwe rafiki wa dunia (tusiipende), bali tuzidi kuimarisha uhusiano wetu na Mungu kila siku (1Yohana 2:15) Tuepukane na tamaa za mwili, tamaa za macho na kiburi cha uzima. Tuimarike katika uchaji, na unyenyekevu wa kweli. Tukiyaishi mafundisho yetu, na kumtambulisha Yesu tuliyembeba kwa ujasiri. Huu ndio utumishi utakaotupa heshima mbele za Mungu (Yohana 12:26) Tunapaswa kuimarika katika Imani, kisha tuzidi sana kuitenda kazi ya Mungu (1Wakorintho 15:58), hakika taabu yetu haitakuwa bure.

Ni mimi mtumishi mwenzako nikibubujikwa na machozi kwa ajili ya kanisa la Mungu. Nakutakia neema na uwezezo kutoka juu katika kuyatenda mapenzi ya Mungu. Upendo wa Mungu, na ushirika wetu katika Roho Mtakatifu uzidi kudumu daima. Mwokozi wetu Yesu adhihirike kwako kwa matendo makuu. Huduma yako iliyokuwa imenyauka ichanue tena kama mti wakati wa masika. Neema ya Bwana wetu Yesu Kristo na ikae pamoja nawe. Amina.


Na: Mwl. Stephen M. Swai
AMKA GOSPEL MINISTRIES INT’L
Simu: +255 713 511 544


MWANAUME KWENYE NAFASI YA "MUME"

Mume ni mwanaume aliyeoa kwa kuzingatia vigezo na taratibu za kijamii, kishria na za kiroho. Mume si rafiki wa kiume (boyfriend), hawara, wa...

Powered By Blogger