Monday, 16 January 2017

MADHARA YA RUSHWA (UFISADI, CORRUPTION, BRIBERY) KWA TAIFA


Mithali 29:4 “Mfalme huithibitisha nchi kwa hukumu; Bali yeye apokeaye rushwa huipindua.”


Rushwa/Ufisadi (Corruption) – Ni kukosa uaminifu na kutumia vibaya mamlaka, au ni matumizi yasiyo halali ya ofisi kwa jili ya kujinufaisha mwenyewe. Mla rushwa (corrupt) ni mtu aliyeamua mwenyewe kutumia nafasi yake ya uongozi, au ofisi kwa manufaa binafsi. Rushwa huwa inatumika kama msukumo wa kupotosha hukumu na kuwatolea wenye haki, haki zao; kisha kuwapa wasiohaki nafasi. Tangu zamani watu maskini, wajane, mayatima walinyimwa haki zao kwa sababu ya rushwa; na jambo hili limekuwa likimuudhi sana Mungu.

Rushwa/ufisadi hubeba sura mbali mbali, inaweza ikawa kwa mfumo wa hongo yaani kutoa fedha au mali kwa ajili ya kushawishi maamuzi Fulani yasiyo halali au sahihih kufanyika. Katika nyakati hizi pia tuna aina nyingine ambayo imekuwa ikisemwa sana na mabinti wanaokwenda kuomba kazi maofisini – Rushwa ya ngono.

Mfumo mwingine ni ule wa kuchota hela kutoka kwenye serikalini kwa kutumia mgongo wa miradi na shughuli mbalimbali za serikali. Au kupunguza hela za matumizi ya serikali na kujiwekea kwa matumizi binafsi. Kutumia ofisi za uma kwa manufaa ya kibiashara binafsi, kujiwekea rasilimali ambazo zilipaswa ziwe za wengi mfano mashamba na viwanja.

Mara nyingi wanyonge na maskini wasio na uwezo wakutoa rushwa ndio huteseka na kuishi maisha magumu, huku wachache wenye fedha wakifanya wanavyotaka. Hali hii ni hatari sana kwa maisha ya watu na taifa kwa ujumla. Zipo sababu nyingi lakini katika makala hii nitataja sababu chache, ni kwa nini rushwa ni hatari kwa taifa:

1. Rushwa hulifarakanisha Taifa na Mungu kwani Mungu anachukizwa sana na Rushwa.
Katika kitabu cha Kumbukumbu la Torati 10:17 tunasoma, “Kwa maana Bwana, Mungu wenu, yeye ndiye Mungu wa miungu, na Bwana wa mabwana, Mungu mkuu, mwenye kuogofya, asiyependelea nyuso za watu, wala hakubali RUSHWA.” Kama Yeye mwenyewe hakubali, basi hawezi kukubaliana nayo. Watu wanapotoa na kupokea rushwa moja kwa moja wanakuwa kinyume cha Mungu asiyependa upendeleo. Maagizo ya Mungu kwa viongozi wote ni:
-        Kuhukumu kwa haki
-        Kuwa na usawa
-        Kutenda mema kwa watu wote


  •  Kusimamia watu kulingana na utaratibu uliowekwa na kukubalika mbele za Mungu.
  •   Kusimama kwa niaba ya Mungu kutoa maagizo yanayostahili kwa watu
  •     Kuyashika maagizo na sheria za Mungu, huku wakijua Mungu ndiye aliyewapa mamlaka.
  •   Anapotokea viongozi wakaenda kinyume na haya yote, wanakuwa wanajisababishia hatia mbele za Mungu. Na kwa sababu Mungu anachukizwa nao, mambo mabaya hayapungui kwao. Magonjwa, majaribu, shida, misiba, na majanga mengi yanaambatana nao. Taifa lenye viongozi kama hawa liko kwenye hatari kubwa kwani kuna uwezekano mkubwa mambo mengi yakaharibika kwa sababu viongozi wamejikita katika kutatua shida zao.
Kwa kinywa cha nabii Isaya Mungu anazungumza juu ya wakuu wa watu wake, Isaya 1:23 anasema, “Wakuu wako ni waasi, na rafiki za wevi; kila mtu hupenda rushwa, hufuata malipo; hawampatii yatima haki yake, wala maneno ya mjane hayawawasilii.” Mungu hapendezwi kabisa na hali hii.
     2. Rushwa hupofusha macho ya viongozi
Ili taifa liweze kuendelea katika eneo lolote ni lazima pawe na viongozi wanaoweza kuona ili kuwapa watu maelekezo ya kuwasaidia; na kufungua fursa kwa wenye uwezo kuzitumia. Viongozi wanapaswa kuziona fursa na changamoto zinazoweza kujitokeza huko tuendako. Mataifa mengi ya kiafrika yanataabika kwa sababu ya mambo ambayo hayakutazamwa ipasavyo na viongozi waliotangulia. Wengi walipopata nafasi walijitazama wenyewe, hawakuwa na wa kuangalia mbele kitakachotokea.

Viwanda vingi vilivyoachwa na wakoloni vilifungwa baada ya miaka michache kwa sababu walioachiwa hawakuweza kuona changamoto ambazo zingejitokeza, hivyo wakakwama baada ya muda mfupi. Na wengine wa sababu ya kujipenda wenyewe wakajilimbikizia vitu na kuua shughuli zote za kuufaidisha uma.

Katika kitabu cha kutoka Mungu anaongea na uongozi wa Israeli kusema, “Nawe usipokee rushwa; kwani hiyo rushwa huwapofusha macho hao waonao, na kuyapotoa maneno ya wenye haki.” Kutoka 23:8. Hapa Mungu anatoa madhara makubwa mawili ya rushwa, yaani kupofusha macho ya waonao na kupotoa maneno ya wenye haki. Maneno ya wenye haki ndiyo huliinua taifa, kama wenye haki wakinyamaza taifa litakuwa kwenye hali ngumu.

Katika Kumbukumbu la Torati 16:19 Mungu anaagiza tena kwa kiongozi, “Usipotoe maamuzi; wala usipendelee uso wa mtu; WALA USITWAE RUSHWA; kwa kuwa rushwa hupofusha macho ya wenye akili, na kugeuza daawa ya wenye haki”.

Kwa hiyo, taifa lenye viongozi wala rushwa ni taifa lenye viongozi wasioona (vipofu) na kama viongozi ni vipofu basin a watu wao wanakuwa vipofu. Hii ni hatari sana kwa taifa, taifa lolote linahitaji viongozi wenye maono katika Nyanja mbalimbali ili liweze kuinuka.

     3. Rushwa husababisha laana
Vilio na manung’uniko ya waliyoonewa na kunyimwa haki zao sio Baraka kwa taifa. Viongozi wanapowaacha watu wakateseka na kuumia bila kuwajali huku uwezekano wa kuwasaidia ukiwepo ni laana. Laana hii huwakalia viongozi na uzao wake na taifa lote kwa ujumla. Baadhi ya viongozi wamewafanyia watu ukatili mgumu sana bila kujua, wakati mwingine kiongozi anaweza kuwaza kwamba ni akili kuwadhulumu watu na kutumia nafasi yake kuwakandamiza watu wa hali ya chini; kimsingi hii ni laana.

Mpango wa Mungu ni kwamba wale waliofanikiwa na wenye mamlaka wawasaidie watu wanyonge. Na huu ndio mfumo wa kiroho unaokubalika mbele za Mungu. Taifa linalowajali wanyonge halikosi kubarikiwa. Katika Yeremia 23:1 Mungu anatoa Ole kwa wachungaji ambao kwa tafsiri nyingine tunaweza kusema “kwa viongozi” , anasema “Ole wao wachungaji, wanaoharibu kondoo za malisho yangu na kuwatawanya! Asema Bwana. Kondoo hapa ni watu wanaoongozwa. Kwa hiyo, tunaweza kusema, “Ole wao viongozi wanaoharibu watu (kwa kupotosha hukumu) na kuwatawanya (kwa kuwakosesha amani).

Isaya 10:1 “Ole wao wawekao amri zisizo za haki, na waandishi waandikao maneno ya ushupavu” Hili nalo linawahusu viongozi kwa maana wao ndio waliopewa dhamana ya kuweka sheria. Kumbe ni lazima waweke sheria au amri za haki na wanaohusika na kuandika waandike vizuri kwa kuzingatia utaratibu aliouweka Mungu.

Neno ‘ole’, sio neno la Baraka. Ni neno linaloonyesha kutakuwa na madhara baada ya muda. Kwa hiyo ni lazima viongozi wajiepushe na rushwa ili kuliepusha taifa na laa (mabaya). Taifa lenye viongozi waliolaaniwa ni taifa ambalo halina mwelekeo mzuri, viongozi waliobarikiwa huinua taifa.

    4. Rushwa hupanda uchungu ndani ya watu, na kuwafanya watu kuchukia taifa lao wenyewe
Uchungu ni kitu kibaya sana kwa watu, uchungu huleta mateso, huchoche malumbano na migomo. Watu wenye uchungu ni rahisi kwenda kinyume na uongozi, na kuleta maafa makubwa.  Taifa lenye watu waliojaa uchungu liko kwenye hatari kubwa sana, kwani watu wengi wanakuwa hawako tayaya

Mungu anataka watu ambao watapenda watu wake wafanikiwe, kwenye Zaburi 15:5 anasema, “Hakutoa fedha yake apate kula riba, Hakutwaa rushwa amwangamize asiye na hatia. Mtu atendaye mambo hayo Hataondoshwa milele.” Hapa tunaona mtu ambaye anawekeza kwa haki, asiyetoa rushwa anakuwa na maisha marefu.

      5. Rushwa kufunga fursa za maendeleo
Taifa lolote lenye watu wanaopenda rushwa, haliwezi kuwa na fursa za kutosha kwa ajili ya watu wake. Sababu kubwa ni kwamba fursa huwa zinaambatana, kwa hiyo kama mtu amefunga fursa moja kwa sababu ya faida binafsi basi anakuwa amefunga fursa nyingine nyingi. Mfano mtu aliyepewa dhamana ya kusimamia shule au kiwanda kisha akakubali kutumia hiyo nafasi vibaya kwa kujiangalia binafsi, akapindua mambo na mwisho kiwanda kikafa. Mtu huyu atakuwa amezuia biashara zilizokuwa zinafanyika kupitia hicho kiwanda, amepunguza uzalishaji, amewafanya watu wakose ajira na kadhalika.

Ili fursa za maendeleo zifunguke ni lazima fursa zilizopo zitumiwe vizuri. Rasilimali watu, fedha pamoja na maliasili ni lazima zitumiwe kwa uaminifu kwa kuzingatia mipango ya maendeleo iliyowekwa vinginevyo baada ya muda kilio cha kukosekana kwa fursa kitaendelea kuwa kikubwa zaidi. Vijana wanapoinuka wakakutana na watu waliojeruhiwa, viwanda vilivyokufa, maduka yaliyofungwa, maliasili zilizotumiwa bila utartibu wanabaki kwenye wakati mgumu.

Siri iliyowafanya walioendelea wakaendelea ni kule kuwa makini na kila fursa iliyojitokeza, baada ya kuzitumia vema hizo fursa ikafika mahali kila siku fursa mpaya zinafunguka, vijana wakizaliwa wanakuta mazingira mazuri yanayowasaidia kuziona fursa mbalimbali. Serikali inahusika moja kwa moja katika kuhakikisha watu wanazitumia vema fursa zinazofunguka.

    6. Rushwa huleta mafarakano na visasi kati ya watu
Watu walioonewa na kunyimwa haki zao, hawawezi kuwa na mahusiano mazuri na wale waliosababisha wao wakapoteza haki zao. Kinachotokea ni roho ya kisasi kujengeka, na kwa sababu ile shida inaingia mpaka kwa watoto basi unakuta jamii nzima inakuwa na hali ya visasi. Wengine watatumia nguvu za uharibifu walizonazo, wengine migomo, wengine nguvu za giza na wengine kutafuta nafasi za uongozi ili kupata fursa ya kulipiza kisasi.

Kuna kauli nimeisikia ikisemwa sana na watu wa hali ya chini kwa watoto wao wanapowasisitiza juu ya swala la shule, utasikia wakisema, “Soma kwa bidii angalau ukifika huko na sisi tutaonekana kuwa watu, siku hizi kama huna mtu huwezi kufika popote”. Bila shaka  hii ni kauli ya mtu anayejiona katika hali ya kutengwa kutokana na umaskini wake. Rushwa ni mbaya sana mioyo ya watu wengi katika nchi zinazoendelea imeharibiwa na rushwa.


7. Rushwa huzuia marafiki na kuongeza maadui.
Taifa lililojaa rushwa haliwezi kuwa na marafiki wengi, kwani baada watu waliokuwa marafiki kugundua kwamba misaada waliyokuwa wanatoa iliwafaidisha wachache na haikuwafikia walengwa wanajeruhika na kuvunja mahusiano. Hili ni dhahiri kabisa mataifa mengi yaliyokuwa yanatoa misaada kwa nchi zinazoendelea yamevunjika moyo kwa sababu wakifuatilia wanakuta shida walitaka kutatua zko palepale.

Yaani barabara walizofadhili zimevunjika, majengo waliyojenga, watu waliiba hela wakajenga chini ya kiwango, masikini waliotumika kutafutia misaada bado hali zao ziko vilevile. Na mengine yanayovunja moyo hata kuliko haya. Mataifa mengi yaliyoendelea wanapenda sana ushirikiano na viongozi waaminifu na wenye uchungu na maisha ya watu.

8. Rushwa hupotosha hukumu na kuvunja utaratibu wa uongozi katika taifa (katiba).
Taifa lenye watu wanaotoa na kupokea rushwa, linakuwa na watu wengi ambao mioyo yao imeathirika na hawawezi tena kutoa hukumu inavyopasa. Wamesoma lakini wanakuwa hawana akili, unakuta kesi ambazo wanaweza kuamua hata watu wa kawaida kwa ufasaha zinawashinda waliosomea. Roho Rushwa inaharibu utaratibu wa uongozi katika taifa.

Kiujumla, Viongozi wanakosa uwezo wa kukaa kwenye nafasi zao, kuna wakati wanapaswa wasema ila wanakaa kimya; kuna wakati wanapaswa wakatae ila wanakubali tu; kuna wakati wanafanya yasiyowapasa. Hili liko dhahiri, kuna mahali ukipita unaweza kusema hivi hapa palikuwa na kiongozi? Swali hili hujitokeza kwa sababu kiongozi hutambulika kwa utendaji wake. Kwa kifupi, Kiongozi aliyekuwepo alikuwa ameuza nafasi yake ya uongozi, akabaki kama pambo tu.

Kwa sababu ya rushwa wakuu wanakosa ujasiri wa kuwakemea wa chini yao, kwanini? Kwa sababu kuna siri wamefichiana. Anaogopa kukemea ili mambo yake yasiwekwe wazi. Kwa hiyo, kwa jinsi hii mfumo mzima wa uongozi unakuwa umevurugika, watu wachache wenye madaraka wanakuwa ndio waamuzi wa kila kitu. Katima inabaki kuwa pambo tu. Taifa lililojaa rushwa ni gumu sana, linakuwa na sheria zisizofuatwa, wanapanga bajeti isiyosimamiwa, wanaweka mipango ambayo haitekelezwi ipasavyo.


9. Husababisha kuinuka kwa viongozi wasio na sifa.
Taifa linaweza kuwa na watu wengi sana wasio na sifa, walioingia kwenye nafasi kwa kuteuliwa au kwa kuchaguliwa kutoana na rushwa. Mwanya huu unapojitokeza unakuwa ndio mlango wa rushwa zaidi na zaidi. Kwa nini? Sababu kubwa ni kwamba watu wasio na uwezo wa kufanya mambo watafuta namna ya kuwafunga vinywa wafuatiliaji, na njia rahisi ni kutoa rushwa/hongo. Kwa jinsi hii taifa linadorora kiuchumi.

Rushwa huwafanya watu wafanye maamuzi yasiyofaa wakati wa uchaguzi, rushwa huwafanya wenye uwezo kukata tamaa hasa walio katika mazingira magumu/walio chini kiuchumi. Taifa linakosa watu wabunifu; wanabaki walewale waliozaliwa katika kambi ya wala rushwa ambao rushwa imeanza kuingia kwenye damu zao tangu mimba ilipotungwa.

Mataifa mengi ya ki-Afrika yamekuwa kwenye wakati mgumu kwa sababu ya baadhi ya viongozi waliopenya nakuingia kwenye nafasi zao kwa njia isiyo halali. Ninaposema viongozi simaanishi maraisi tu namaanisha kila mtu mwenye nafasi kwenye eneo Fulani, iwe ni serikalini au sekta binafsi.


10. Hupindua kweli, hivyo kulipindua taifa na kuliletea aibu.
Katika Mithali 29:4 tunasoma jambo la ajabu sana. Neno linasema “Mfalme (kiongozi) huithibitisha nchi kwa hukumu; Bali yeye apokeaye rushwa huipindua.” Kumbe mapinduzi hayafanywi na wanasiasa tu, hata wala rushwa nao wana uwezo wa kuipindua nchi. Wanaipinduaje? Nafikiri ni kwa njia ya kufanya mambo yaende ndivyo sivyo:


  •   Kutoka kwenye kuwa nchi ya amani na kuwa nchi ya vita na migogoro
  •    Kutoka kwenye kuwa nchi ya kupendana kwenda kwenye nchi ya chuki na visasi
  •     Kutoka kwenye nchi inayoendelea kuwa nchi anayodaiwa
  •   Kutoka kwenye nchi inayojitegemea kwenda kwenye nchi tegemezi na mapinduzi mengine
  •         Kutoka kwenye nchi inayoheshimiwa kwenda kwenye nchi inayodharauliwa
Kumbuka dhambi ni aibu ya taifa. Katika Mithali 14:34 tunasoma, “Haki huinua taifa; Bali dhambi ni aibu ya watu wo wote.” Kwenye mstari huu tunapata pande mbili za taifa:

-        Upande wa Haki, pale ambapo watu wanafanyiwa mambo kwa haki, hakuna anayemwonea mwingine, rasilimali zinatumika kwa usawa na watu wapewa wanayostahili. Hapa tunaambiwa taifa huinuka (Mafanikio hutokea)
-        Upande wa pili tunakuta dhambi (ikiwepo dhambi ya rushwa ambayo ni dhambi ya karibu sana kwa viongozi na wenye mamlaka). Hapa tunaambi ni aibu ya taifa. Mataifa mengi ya Afrika yanasemwa vibaya kwa sababu ya Rushwa.

        11. Viongozi wanakosa nguvu ya ushawishi kwa watu wao.
Mara nyingi maswala ya rushwa au ufisadi hufanyika kwa siri, ila inapotokea hiyo roho ikaendelea kudumu kwa muda mrefu, uovu wote uliofanyika kwa siri hufichuka na mambo yote huwa wazi kwa watu. Hapo ndipo tafsiri na sura ya viongozi hubadilika kabisa ndani ya watu. Watu huanza kuwaona viongozi kama wabinafsi na watu wasio na uwezo wa kujizuia. Hapo inakuwa kila watalolisema linahusishwa moja kwa moja na tabia yao ya kupenda rushwa/ufisadi.

Viongozi waaminifu wanakuwa wanapendwa sana na watu, wanaweza kuwaambia watu mambo na wakawaelewa. Watu wanawaona ni watu wenye uwezo mkubwa wa kuweza kutatua matatizo yao, sio kuongeza matatizo. Viongo kama Mwalimu Julius K. Nyerere raisi wa Kwanza wa Jamhuru ya Muungano wa Tanzania walikuwa na ushawishi mkubwa kwa sababu ya kuchukia rushwa.

Taifa lenye viongozi mafisadi/wala rushwa linakuwa na viongozi wasioweza kusikilizwa na watu wao. Wanaweza kuitisha mikutano watu wasihudhurie. Ila kama viongozi ni wema, waaminifu, waadilifu na wanaofanya mambo kwa haki, wanaoongozwa wanakuwa na upendo wa dhati kabisa kwao. Na hivi ndivyo Mungu ameweka, kwamba wenye mamlaka wapewe heshima.

Waebrania 13:17 inasema, “Watiini wenye kuwaongoza, na kuwanyenyekea; maana wao wanakesha kwa ajili ya roho zenu, kama watu watakaotoa hesabu, ili kwamba wafanye hivyo kwa furaha wala si kwa kuugua; maana isingewafaa ninyi.” Heshima hii ni kwa watu wale wanaotoa muda wao kwa ajili ya watu wanaowaongoza. Kwa hiyo kama kiongozi ni fisadi hawezi kuheshimiwa na watu wake, nguvu yake ya ushawishi inapungua na hapo taifa liko hatarini.

12. Rushwa huuharibu ufahamu
Katika kitabu cha Mhubiri 7:7 tunasoma, “Kweli jeuri humpumbaza mwenye hekima, Na rushwa huuharibu ufahamu.” Hapa neno hili linazungumza moja kwa moja kwamba rushwa huuharibu ufahamu. Ni kweli kabisa, kuna wakati ukifuatilia baadhi ya maamuzi yaliyofanywa na viongozi wala rushwa (Corrupt leaders) unaweza kushangaa sana. Baadhi ya maamuzi wanafanya bila ufahamu kabisa.

Ufahamu ulioharibika ni ule ambao haufanyi kazi ipasavyo, ni kama mtu anajua ila hajui. Ufahamu ulioharibika kwa tafsiri nyingine ni upumbavu. Akili zinakuwa zimepumbazwa kwa rushwa, ufahamu umepoteza mwelekeo. Utakuta kiongozi anajua kabisa ujenzi wa miundimbinu Fulani ni kwa ajili ya faida ya sasa nay a baadaye, lakini atathubutu kutumia fedha za miundombinu kwaajili ya mambo yake binafsi. Hii ni kwa sababu ya ufahamu ulioharibika.

Hitimisho
Naamini kupitia makala hii utakuwa umepata kitu cha kukusaidia katika lile unaloweza kufanya katika kupiga vita rushwa katika bara letu la Africa. Ili nchi zetu za kiafrika zipige hatua kiuchumi, kisiasa na kijamii ni lazima iwe na watu wanaoichukia rushwa ili kuepukana na madhara yote yaliyotajwa hapo juu. Najua kwa msingi huu wa maneno kutoka kwenye Biblia Takatifu ambacho ni kitabu kinachotumiwa na wengi duniani kote, kuna mambo ambayo yamekuwa wazi kuliko ilivyokuwa mwanzo.

Ikiwa wewe ni kiongozi uliyeteuliwa au kuchaguliwa, au unasimamia kampuni binafsi au vyovyote ulivyo, nina hakika kila mtu ni kiongozi katika eneo lake; au wewe na raia mwema wa taifa Fulani, nakusii usimame katika nafasi yako kuhakikisha mbegu ya rushwa haiendelei kumea na kuifunika nchi yako.

Kila mtu ana nafasi katika kutokomeza adui huyu anayejulikana kwa majina mengi. Wengine humwita Corruption/bribe, wengine rushwa, wengine hongo, wengine takrima, wengine kitu kidogo na mengine mengi. Kimsingi hawa wote ni watoto wa baba mmoja na kazi yao na kuleta umaskini wa wengi huku wachache wakinufaika.

Mungu ibariki Tanzania! Mungu ibariki Afrika!

Na Mwl. S.S.Michael
Simu: 0713511544 (Whatsapp)




MWANAUME KWENYE NAFASI YA "MUME"

Mume ni mwanaume aliyeoa kwa kuzingatia vigezo na taratibu za kijamii, kishria na za kiroho. Mume si rafiki wa kiume (boyfriend), hawara, wa...

Powered By Blogger