Monday, 30 July 2018

JIFUNZE KUNYENYEKEA

UNYENYEKEVU (HUMBLENESS/HUMILITY)

Dunia imejaa watu wanaotamani ukuu, utajiri na umaarufu; huzuni ni kwamba wengi hawajaelewa siri iliyopo kwenye kuinuliwa kwa mtu. Jitihada za kuonekana (kuwa maarufu), kuwa na fedha au mengine zimewakaa sana wanadamu. Na hii ni kawaida ya wanadamu, tumeumbwa lili tuishi kwa utukufu wa Mungu. Mafanikio yetu, hasa yanayotokana na Mungu yanaonesha utukufu wa Mungu.

Mambo ya msingi ya kujua:

A. Utajiri na heshima ya kweli hutokana na Mungu: Maandiko katika 1 Samweli 2:7 yanasema, "Bwana hufukarisha mtu, naye hutajirisha; Hushusha chini, tena huinua juu." Tena katika Mithali 8:18 tunasoma, "Utajiri na heshima ziko kwangu, Naam, utajiri udumuo, na haki pia."
Hivyo bila Mungu mtu akipata utajiri, hauwezi kuwa wa kudumu. Tena utajiri unaoambatana na heshima ni ule unaotoka kwa Mungu.
Kwenye Mithali 22:4 inatuweka sawa zaidi "Thawabu ya unyenyekevu ambao ni kumcha Bwana Ni utajiri, na heshima, nayo ni uzima." 

Kunyenyekea (Kumcha Mungu), kumeelezwa kuwa na matokeo makubwa matatu:
Utajiri: kumiliki au kuwa na mali nyingi
Heshima: kuwa na thamani kwa watu wanaokuzunguka
Uzima: kuwa na uhai au maisha.

Jumla ya mambo haya ni maisha bora (Maisha ya mafanikio). Mtu yeyote ambaye ni mnyenyekevu mbele za Mungu ana nafasi kubwa ya kuweza kufanikiwa katika Mungu.

Utajiri wa kweli hutokana na baraka za Mungu. Mithali 10:22 "Baraka ya Bwana hutajirisha, Wala hachanganyi huzuni nayo." Tukinyenyekea kwake atatuinua. 1 Petro 5:6 Basi nyenyekeeni chini ya mkono wa Mungu ulio hodari, ili awakweze kwa wakati wake;

B. Kufanya kazi kwa bidii na uaminifu ni sehemu ya unyenyekevu. Mtu aliyejaa kiburi, mbinafsi hawezi kufanya kazi kwa mafanikio. Mtu mwenye bidii katika kazi ana nafasi kuwa sana ya kufanikiwa (wakati mwingine hata kama hana uhusiano mzuri na Mungu). 

Shida ya kufanikiwa nje ya Mungu, ni maisha kuwa katika hatari. Haiwezekani kudumu katika utajiri, heshima na uzima bila kuwa na Mungu. Labda mtu aamue kuyauza maisha yake kwa shetani, napo shetani ni mwivi, aibaye na kuharibu na kuchinja (Yohana 10:10)

C. Kunyenyekea na kuwaheshimu wazazi kunaleta mafanikio na maisha marefu. Kumb. 5:16 Waheshimu baba yako na mama yako; kama Bwana, Mungu wako, alivyokuamuru, siku zako zipate kuzidi, nawe upate kufanikiwa katika nchi upewayo na Bwana, Mungu wako.

Watu wengi wamekwama kwa sababu ya kuonyesha kiburi kwa wazazi wao. Ni kweli unaweza kuwa umesoma kuliko wao, au una imani kuliko wao au umewazidi kiuchumi; bado ni haki yao kupata heshima kutoka kwako. Uwasikilize na utii katika yale yanayompendeza Mungu. Kushindana na wazazi hakuna baraka, ni laana.

D. Wazazi wa kiroho nao ni watu wa muhimu sana (Paulo anawaita wazee au watu waliotutangulia katika Imani). Mchungaji au mtu yeyote ambaye Mungu amemweka mbele yako akusaidie katika maisha yako ya kiroho, huwezi kuishi naye bila unyenyekevu. 

Yohana 13:14 "Basi ikiwa mimi, niliye Bwana na Mwalimu, nimewatawadha miguu, imewapasa vivyo kutawadhana miguu ninyi kwa ninyi." Hapa Yesu anatufundisha somo kubwa la kunyenyekeana sisi kwa sisi. Hii ndiyo njia ya kuwa wakuu kuliko wengine. Yesu anasema mkuu lazima awe mtumwa wa wengine. Marko 10:44 na mtu anayetaka kuwa wa kwanza wenu, atakuwa mtumwa wa wote.

E. Kunyenyekea kwa viongozi ni njia ya kumweshimu Mungu aliyewaweka katika hiyo mamlaka. Kama umeajiriwa au unaishi katika nchi au eneo fulani. Unyenyekevu ndiyo njia ya kupata kibali kwa wakuu. Ajikwezaye hushushwa. Uwe mnyenyekevu huku ukitimiza majukumu yako kwa moyo. Ukiona watu wananyenyekea kwa raisi usiwashangae, wameng'amua siri ya kufanikiwa. Kunyenyekea si kujipendekeza. Ni kumpa heshima anayestahili heshima.

Mwisho Petro anasema"Waheshimuni watu wote. Wapendeni ndugu. Mcheni Mungu. Mpeni heshima mfalme."1 Petro 2:17 

JE, UNATAKA KUFANIKIWA KATIKA MUNGU? JIFUNZE KUNYENYEKEA. UTAFANIKIWA.

Na. Mwl. S.S.Michael
Simu: 0713511544 (Whatsapp)

Sunday, 8 July 2018

SOTE TUPIGE KELELE


 "ZIMWI HILI HALIJAFA"


Ama kweli rushwa zimwi, tena zimwi kwelikweli
Lazidi hata ukimwi, upungufu kinga za mwili
Kama moto halizimwi, kila kona watu chali
Zimwi linatutafuna, sote tupige kelele

Halichomwi Kwa mkuki , kwa risasi halitoki
Chunguni halipikiki, ni gumu halikatiki
Adui wa kila haki, kuchafua halichoki
Zimwi linatutafuna, sote tupige kelele

Tena halijabagua, kwa yeyote linapita
Rangi yake yavutia, kila mtu kumvuta
Mjini kijiji pia, kotekote talipata
Zimwi linatutafuna, sote tupige kelele

Wengi walio kitini, wamekwisha kuvamiwa
Ni wema sana machoni, moyoni ni kama chawa
Aingiapo mwilini, hataki kuondolewa
Zimwi linatutafuna, sote tupige kelele

Nyangumi pia dagaa, wote limewafikia
Mashilingi wayazoa, nyumba zao kujengea
Hoja wanazozitoa, uongo tamu kolea
Zimwi linatutafuna, sote tupige kelele

Wako kama hayawani, hawataki makatazo
Kila kitu mfukoni, wanazidisha ujazo
Utu kwao ndio nini, Rushwa kwao ndiyo chanzo
Zimwi linatutafuna, sote tupige kelele

Wangine kiomboleza, wao kwao ni tulizo
Hukumu kuigeuza, hilo kwao si tatizo
Haki nazo kuziuza, kila kona ni uozo
Zimwi linatutafuna, sote tupige kelele

Yatima hata wajane, wamekuwa kama ngazi
Wanapopanda  wengine, kukanyagwa ndiyo kazi
Wakisema wayanene, mwisho wake ni machozi
Zimwi linatutafuna, sote tupige kelele

Huko nako barabara, nao wamo mtegoni
Wamebaki na mkwara, nacho kidogo pembeni
Japo wana mshahara, wataka na mkononi
Zimwi linatutafuna, sote tupige kelele

Kanisani ‘sikitini, zimwi linajipenyeza
Tuulize kulikoni, nako tume kuchunguza
Hawa watu wa Imani, Mola hajawatuliza?
Zimwi linatutafuna, sote tupige kelele

Masikini hatiani, matatani kibindoni
Makosani hukumuni, mtieni gerezani
Nguvuni afanye nini, mhaini wa kitini?
Zimwi linatutafuna, sote tupige kelele

Hili zimwi tangu kale, halina wa kulitaka
Sio hawa wala wale, kauli ni toka toka
Kwa hatua na kelele, zimwi hili tatimka
Zimwi linatutafuna, sote tupige kelele

Zimwi hili ni laana, lachafua nchi yote
Tena halina maana, adui wa watu wote
Linaleta kuumana, na vilio kotekote
Zimwi linatutafuna, sote tupige kelele

Hongera kwa wateule, wapigao makelele
Maisha yasiwe yale, ya hadithi tangu kale
Uzalendo utawale, tamaa tutupe kule
Zimwi linatutafuna, sote tupige kelele

Tusitazame usoni, tukitaka ua nyani
Wahuni na waumini, vitini uraiani
Bungeni nako chamani, mkoani wilayani
Zimwi linatutafuna, sote tupige kelele

Majumbani mashuleni, televisheni redioni
Barabani mtaani, mjini na vijijini
Jijini mtandaoni, Gazetini  vitabuni
Zimwi linatutafuna, sote tupige kelele

Mahakamani barazani, Jeshini sipitalini
Ofisini mashambani, makampuni sokoni
Mashuleni na vyuoni, kusini kaskazini
Zimwi linatutafuna, sote tupige kelele

Hata nako vitabuni, zimwi hili ni chukizo
Chukizo kwa Maanani, kwalo hataki mchezo
Hasa wale wa enzini, wasiotaka katazo
Zimwi linatutafuna, sote tupige kelele

Chonde chonde wanakwetu, tusimmunye maneno
Sote tubebe mtutu, tuanzishe fungamano
Nchi yetu haki zetu, tusongeshe mpambano
Zimwi linatutafuna, sote tupige kelele

MWANAUME KWENYE NAFASI YA "MUME"

Mume ni mwanaume aliyeoa kwa kuzingatia vigezo na taratibu za kijamii, kishria na za kiroho. Mume si rafiki wa kiume (boyfriend), hawara, wa...

Powered By Blogger