"ZIMWI HILI HALIJAFA"
Ama kweli
rushwa zimwi, tena zimwi kwelikweli
Lazidi
hata ukimwi, upungufu kinga za mwili
Kama moto
halizimwi, kila kona watu chali
Zimwi linatutafuna, sote tupige kelele
Halichomwi
Kwa mkuki , kwa risasi halitoki
Chunguni
halipikiki, ni gumu halikatiki
Adui wa
kila haki, kuchafua halichoki
Zimwi linatutafuna, sote tupige kelele
Tena
halijabagua, kwa yeyote linapita
Rangi
yake yavutia, kila mtu kumvuta
Mjini
kijiji pia, kotekote talipata
Zimwi linatutafuna, sote tupige kelele
Wengi
walio kitini, wamekwisha kuvamiwa
Ni wema
sana machoni, moyoni ni kama chawa
Aingiapo
mwilini, hataki kuondolewa
Zimwi
linatutafuna, sote tupige kelele
Nyangumi
pia dagaa, wote limewafikia
Mashilingi
wayazoa, nyumba zao kujengea
Hoja
wanazozitoa, uongo tamu kolea
Zimwi linatutafuna, sote tupige kelele
Wako kama
hayawani, hawataki makatazo
Kila kitu
mfukoni, wanazidisha ujazo
Utu kwao
ndio nini, Rushwa kwao ndiyo chanzo
Zimwi linatutafuna, sote tupige kelele
Wangine
kiomboleza, wao kwao ni tulizo
Hukumu kuigeuza,
hilo kwao si tatizo
Haki nazo
kuziuza, kila kona ni uozo
Zimwi linatutafuna, sote tupige kelele
Yatima
hata wajane, wamekuwa kama ngazi
Wanapopanda wengine, kukanyagwa ndiyo kazi
Wakisema
wayanene, mwisho wake ni machozi
Zimwi linatutafuna, sote tupige kelele
Huko nako
barabara, nao wamo mtegoni
Wamebaki
na mkwara, nacho kidogo pembeni
Japo wana
mshahara, wataka na mkononi
Zimwi linatutafuna, sote tupige kelele
Kanisani
‘sikitini, zimwi linajipenyeza
Tuulize
kulikoni, nako tume kuchunguza
Hawa watu
wa Imani, Mola hajawatuliza?
Zimwi linatutafuna, sote tupige kelele
Masikini
hatiani, matatani kibindoni
Makosani
hukumuni, mtieni gerezani
Nguvuni
afanye nini, mhaini wa kitini?
Zimwi linatutafuna, sote tupige kelele
Hili
zimwi tangu kale, halina wa kulitaka
Sio hawa
wala wale, kauli ni toka toka
Kwa hatua
na kelele, zimwi hili tatimka
Zimwi linatutafuna, sote tupige kelele
Zimwi
hili ni laana, lachafua nchi yote
Tena
halina maana, adui wa watu wote
Linaleta
kuumana, na vilio kotekote
Zimwi
linatutafuna, sote tupige kelele
Hongera
kwa wateule, wapigao makelele
Maisha
yasiwe yale, ya hadithi tangu kale
Uzalendo
utawale, tamaa tutupe kule
Zimwi linatutafuna, sote tupige kelele
Tusitazame
usoni, tukitaka ua nyani
Wahuni na
waumini, vitini uraiani
Bungeni
nako chamani, mkoani wilayani
Zimwi linatutafuna, sote tupige kelele
Majumbani
mashuleni, televisheni redioni
Barabani
mtaani, mjini na vijijini
Jijini
mtandaoni, Gazetini vitabuni
Zimwi linatutafuna, sote tupige kelele
Mahakamani
barazani, Jeshini sipitalini
Ofisini
mashambani, makampuni sokoni
Mashuleni
na vyuoni, kusini kaskazini
Zimwi linatutafuna, sote tupige kelele
Hata nako
vitabuni, zimwi hili ni chukizo
Chukizo
kwa Maanani, kwalo hataki mchezo
Hasa wale
wa enzini, wasiotaka katazo
Zimwi linatutafuna, sote tupige kelele
Chonde
chonde wanakwetu, tusimmunye maneno
Sote
tubebe mtutu, tuanzishe fungamano
Nchi yetu
haki zetu, tusongeshe mpambano
Zimwi linatutafuna, sote tupige kelele
No comments:
Post a Comment