Saturday, 21 March 2020

MAARIFA YA MUNGU HULETA MAHUSINO MAZURI KATIKA FAMILIA


Maarifa ni uwezo wa kutumia ufahamu ili kusababisha mabadiliko au matokeo mazuri au mafanikio.  Unaweza ukawa ni ufahamu wa kiroho au ufahamu wa kawaida wa kibinadamu. Kuwa na ufahamu tu hakutoshi, bali ni lazima mtu aweze kuutumia huo ufahamu vizuri kwa ajili ya maisha ya kila siku. Chanzo cha maarifa yote ni uchaji mbele za Mungu (Mithali 1:7) Yaani kuwa na hofu ya Mungu kunakodhihirika katika ibada na utii katika neno lake. Katika maisha yetu yapo mengi yanayohitaji maarifa na hekima ya Mungu. Maarifa huleta hekima na hekima hutuwezesha kuishi vizuri na watu, hivyo kuwa na maisha ya furaha na amani.

Katika Muhubiri 11:8-9 Maandiko yanasema,

Naam, mtu akiishi miaka mingi, na aifurahie yote; lakini na azikumbuke siku zijazo za giza, kwa maana zitakuwa nyingi…..Wewe kijana, uufurahie ujana wako, na moyo wako ukuchangamshe siku za ujana wako, ukaziendee njia za moyo wako, na katika maono ya macho yako, lakini ujue wewe ya kwamba kwa ajili ya hayo yote Mungu atakuleta hukumuni.”

Katika mistari hii tunajifunza kwamba ni mpango wa Mungu tuifurahie miaka yote ya maisha yetu, ikiwepo miaka ya utoto, ujana, utu uzima na uzee. Swali langu ni kwamba, “Ni kwa nini vijana na watoto wengi wanaishi maisha ya huzuni, majuto, maumivu makali moyoni, migogoro, chuki, dhiki nk? Katika kutafakari nikagundua kwamba ipo shida kubwa kwenye mahusiano kati ya watoto/vijana na wazazi/walezi. Watoto wengi wamewaumiza wazazi/walezi wao kwa tabia zao mbaya za dharau na dhambi, kwa upande mwingine nao wazazi/walezi wamewaumiza watoto/vijana kwa kutotimiza wajibu wao na kuwatendea mabaya.

Tena katika Hosea 4:6 Mungu anasema, “Watu wangu wanaangamizwa kwa kukosa maarifa; kwa kuwa wewe umeyakataa maarifa, mimi nami nitakukataa wewe, usiwe kuhani kwangu mimi; kwa kuwa umeisahau sheria ya Mungu wako, mimi nami nitawasahau watoto wako.” Kukosa maarifa ya Mungu katika kujenga mahusiano ya kifamilia imekuwa ni tatizo kubwa kwa dunia, katika kizazi hiki. Kwa sababu hiyo shetani anazidi kuangamiza kizazi hiki kwa kasi sana.

Kwenye isaya Isaya 5:13 tunasoma matokeo mengine mabaya sana yanayoletwa na kukosa maarifa ya ki-Mungu, hapo tunasoma, “Kwa sababu hiyo watu wangu wamechukuliwa mateka, kwa kukosa kuwa na maarifa; na watu wao wenye cheo wana njaa, na wengi wao waona kiu sana.” Kumbe kwa kukosa maarifa ndipo tunaweza kuona jinsi ambavyo kizazi hiki kimeingia katika uteka wa Ibilisi kupitia mifumo ya kisasa ya maisha. Maeneo mengi watu wanalia kuhusu tabia za watoto wa kizazi hiki.

Wazazi/walezi wamekuwa na wakati mgumu sana katika malezi ya watoto wao. Hapa dawa ni Mungu aingilie kati, maombi na sala pamoja na kuwekeza kwenye kuwajaza maarifa ya Mungu ndilo suluhisho la kudumu. Uteka hauvunjiki kwa vikao na adhabu, au kutishiwa kufungwa gerezani; Mungu ndiye mwenye uwezo wa kuwaweka huru waliosetwa katika mateka ya Ibilisi.

Katika Luka 4:18 Yesu anasema, “Roho wa Bwana yu juu yangu, Kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, Na vipofu kupata kuona tena, Kuwaacha huru waliosetwa” Watoto/vijana wetu wengi wanahitaji mguso wa Mungu watoke katika vifungo vilivyowafunga. Nimeshuhudia matukio mengi katika shule ambazo nimepita, watoto wengi watukutu wanakuwa wana uvamizi wa kipepo ndani yao, si wao katika hali ya kawaida. Kwa maombi yetu na jitihada zetu za kuwafundisha ili wajae maarifa ya kiMungu, ndivyo vitakavyoleta mapinduzi.

Shetani anashughulika kuwazuilia watoto/vijana maarifa ya Mungu ili apate kuwachota kwa urahisi kila siku. Katika Mithali 1:7, tunasoma,  “Kumcha Bwana ni chanzo cha maarifa” Ukiangalia katika kizazi hiki watoto na vijana wengi wamejaa mambo machafu sana, haya mambo ndiyo yanayochafua kabisa mahusiano na wazazi na kuwafanya watoto/vijana waingie kwenye uteka wa Ibilisi. Maswala ya mitandao yamechochea sana uasherati kwa kizazi hiki, siku hizi ni kawaida kukuta binti mdogo waa shule ya msingi ameshaanza maswala ya mapenzi.

Kwenye Mithali 1:28-29 tunaona matokeo mengine mabaya YA kuyakataa maarifa ya Mungu, Neno linasema, “Ndipo watakaponiita, lakini sitaitika; Watanitafuta kwa bidii, wasinione. Kwa kuwa walichukia maarifa, Wala hawakuchagua kumcha Bwana.” Hakuna mwanadamu asiyemwitaji Mungu katika mambo mbalimbali ya maisha yake. Hapa tunaona hali ya hatari inayojitokeza kizazi kinapokuwa na watu walioyakataa maarifa ya Mungu. Kwanza maombi hayatasikiwa na Mungu, pili, Mungu hawezi kuonekana wakati anahitajika. Hivyo ni lazima kila mtu akajua ana wajibu wa kutafuta maarifa ya Mungu ili kwa hayo tuweze kufanya mambo kwa hekima na ufahamu mzuri.

Wito wangu kwa wazazi, waalimu, viongozi, mitume, wachungaji, manabii, jamii na serikali ni kwamba kila mmoja aiangalie nafasi yake. Tuna jukumu la kuhakikisha kwamba watoto na vijana wetu wanazidi kupata maarifa ya Mungu,wanapoendelea kusoma katika elimu mbalimbali. Tusipuuze mambo ya Mungu; vipindi vya dini mashuleni vipewe nafasi yake. Watoto na vijana wasisitizwe kwenda kwenye nyumba za ibada. Vifaa vya kujifunzia elimu ya kiroho navyo vipatikane kwa wingi. Tena kila mmoja wetu awe mfano bora kwa watoto na vijana wetu. Vijana nao wawe tayari, na waamue kuwekeza muda wao katika kujifunza. Wawaheshimu viongozi na waalimu wa kiroho kama inavyowapasa. Hili litadumisha mahusiano kati yao na Mungu, kisha kati yao na wazazi/walezi.

Mungu awabariki,

Mwl. Stephen Swai
Simu: +255713511544

JINA LA YESU KRISTO NI ZAIDI YA MAJINA YOTE, UVIKO - 19 (CORONA) ISIWE TISHIO

USIOGOPE! USIOGOPE! USIOGOPE!

Hapa duniani yapo mambo mengi ya kuogopesha, ya kukatisha tamaa, ya kuumiza, hata ya kutufanya tusione kabisa maana ya maisha haya tunayoishi. Katika historia pia yalishatokea matukio ya kutisha, tukikumbuka mambo kama Sunami, Septermber 11, huko Marekani, vimbunga, matetemeko ya ardhi kwa majina yake; vita vya kwanza na vya pili vya dunia; magonjwa kama vile Ebola, UKIMWI, Kansa, na mengine yamekuwa tishio. Mambo haya yalihusisha nguvu za asili, utendaji wa wanadamu na mengine yalisababishwa na vijidudu visivyoweza hata kuonekana (Virusi, bakteria, na vingine). 

Ni Jambo la kushangaza kuona virusi, ambavyo ni wadudu wasioonekana, kuleta taharuki na mtikisiko mkubwa duniani kote.  Virusi vya HIV vimeitikisa dunia kwa muda mrefu sasa; virusi vya Ebola, na sasa hivi tunatikiswa na virusi vinavyosababisha ugonjwa wa UVIKO - 19 (COVID - 19), yaani virusi vya CORONA (CORONA VIRUS).  Ninachotaka kusema hapa ni nini? Nataka kusema kwamba udogo wa virusi hauvipunguzii uwezo wake wa kuleta madhara. Tena uwezo wake unachangiwa zaidi na umbile lake, ijapokuwa ni dogo. Virusi vya CORONA vinasemekana kuwa vina umbo la taji ya kifalme. Umbo lake linasababisha virusi hivi viweze kusambaa kwa haraka kutoka kwa mtu mmoja kwenda kwa mwingine. Madhara yake yameelezwa kuendelea kuwa makubwa siku kwa siku. Hivyo, kama hatuna msimamo thabiti wa imani ni lazima mtikisiko huu utuletee madhara makubwa.

Virusi hivi viligunduliwa na kuanza kusambaa katika mji wa Wuhan huko China. Baada ya muda mfupi usiozidi miezi mitatu tangu vigunduliwe, virusi hivi viliweza kuigusa dunia nzima. Nchi zaidi ya 114 zilikuwa zimeripotiwa kuwa na waathirika wa virusi hivi; huku China, Italia, na Marekani zikiongoza kwa kuwa na waathirika wengi zaidi. Baadhi ya nchi za Afrika nazo zimeripotiwa kuwa na visa vya watu walioambukizwa virusi hivi. Nchi kama Kenya, Tanzania, Afrika Kusini, Jamhuri ya Demokrasia ya Kongo, Ghana na nyinginezo. Hakika UVIKO -19 imaitikisa dunia. Ni ukweli usiopingika kwamba hofu na mashaka vimewajaa watu wa kila taifa katika dunia hii. Wengi hawana uhuru tena hata wa kutembea hapa na pale, shule zimefungwa, michezo imesitishwa, kumbi zimefungwa, mikusanyiko imekatazwa nk. Hii yote ni kuonyesha jinsi ambavyo hofu imetanda kwa wanadamu.

  Leo nataka nikuletee habari njema. Na nianze kwa kukuuliza "YANINI KUOGOPA?" Unaweza kunijibu tu kirahisi kwamba unaogopa KIFO. Ni kweli kifo ni kitu cha kuogopesha na hakuna mtu anayependa kufa. Ila jiulize tangu dunia iwepo ni wangapi wamekufa? Jibu ni wengi, hawahesabiki. Kifo kimekuwepo, kipo na kitazidi kuwepo. Habari njema ni hii "TUNAYE YESU KRISTO ALIYESHINDA KIFO NA MAUTI" Yeye ni zaidi ya kila kitu. Jina lake liko juu ya majina yote. Yaani liko juu ya jina la Uviko-19 na mengineyo yote. Tukimwamini Yeye tuna uhakika wa kuishi milele. Yeye ni Alfa na Omega, wa kwanza na wa mwisho. Kwa kupigwa kwake sisi sote tumepata kupona (Isaya 53:5) Kila anayemwana Yesu Kristo hana haja ya kuogopa, Yesu ndiye mkombozi na mwokozi wa maisha yetu.

Ndugu zangu, hatuna haja ya kuogopa ugonjwa huu wa UVIKO-19, tuchukue tahadhari kama tunvyoelekezwa na wataalamu lakini tusiogope kwani Mungu wetu zaidi ya kila kitu. Aliyeko ndani Yetu ni mkuu kuliko walio nje. Maandiko yanasema Kwa Jina lake dunia nzima inapata kuokolewa (Matendo 4:12) Ni vema tukamwamini Mungu kuliko kuogopa. Shetani asitujaze hofu, tujue kwamba uhai wetu uko mikononi mwa Mungu. Anayetulinda usiku na mchana ni Mungu peke yake, hatuwezi kujilinda wenyewe. Nirudie tena, "Hatuna haja ya kuogopa" tuhakikishe tu kwamba tuna ushirika mzuri na Mungu, tuombe kwa bidii na kuendelea kumtumaini Mungu. Hakuna haja ya kukosa tumaini na kuona kwamba huwezi kuishi tena. Kirusi cha KORONA si mwamuzi wa maisha yetu. Mwamuzi wa mwisho wa maisha yetu ni Mungu aliyetuumba.

Katika jitihada za wanadamu kutafuta tiba ya kutibu ugonjwa huu, hakujawa na matumaini ya kutosha bado. Japo kuna chnjo za aina mbalimbali zimegunduliwa, hakuna hata moja inayoweza kuaminiwa kwa asilimia mia moja. Hii inathibitisha kwamba ni Mungu peke yake anayeweza kutulinda na kutuhifadhi salama mbele ya mjumbe huyu wa shetani aliyetumwa kuitawala dunia. Ni lazima tukatae kukaa chini ya uweza wa kitu chocho, na tuamue kukaa chini ya uweza wa Mungu peke yake. Kwa mwamini wa kweli Uviko-19 haliwezi kuwa tatizo la kusababisha kupoteza matumaini. Bado aliyeanzisha maisha yetu hapa duniani yuko hai na anaweza kutulinda. (Zaburi 127:1)

Mwisho niseme hizi ni nyakati za mwisho, yapo mengi ya kututikisa, huu ni mwanzo tu wa uchungu. Tunapoelekea yatatokea mengine mazito zaidi. Yote haya yalitabiriwa katika maandiko (Mathayo 24), matetemeko, vita, magonjwa, na mengine. Wapendwa ni muda wa kujiandaa, Yesu yu karibu kurudi. Huu si muda wa kuendelea kukusanya mali na kumsahau Mungu, si muda wa kuendekeza mijadala ya kidini isiyo na faida, wala si muda wa kuwaangalia watu; ni muda wa kujichunguza kila mmoja na nafsi yake. Kila mmoja atasimama mbele ya kiti cha hukumu peke yake. Wahubiri: huu si muda wa kuhubiri ili kupata fedha, tena si muda wa kufundisha mafanikio ya kimwili; ni muda wa kusahau nafsi zetu na kuwa dhabihu kwa ajili ya kanisa la Mungu na ulimwengu kwa ujumla.

Tunaelekea kwenye nyakati ambazo dunia inahitaji faraja kutoka kwa Mungu. Na faraja hiyo ni lazima ipitie kwa kanisa lake (yaani mimi na wewe). Kanisa linakwenda kuwa mahali pa makimbilio kwa watu waliojikuta wanaabudu mashetani wakifikiri wanamwabudu Mungu. Utatokea ufunuo usio wa kawaida baada ya siku hizi chache, macho ya wengi yataona nuru lakini waliopewa nuru wengi watakuwa wamepoteana. Tusiviangalie vya dunia hii na kusahau ile amana tuliyowekewa na Mungu kwa ajili ya watu wake. Nafasi ya mtumishi wa Mungu katika dunia hii ni kubwa, japo watu wengi wanafanya mchezo na utumishi. Leo ni Uviko - 19 (Korona) lakini kesho hatujui ni nini kitatokea. Tusimame imara, tusiogope, tuishi kwa kumtegemea Mungu wala tusiangali vitisho vya shetani; hapa duniani hatuna mji udumuo, tuko kwa kitambo kidogo tu.

Nakuombea Mungu akulinde na akuepushe na ugonjwa wa UVIKO 19 (COVID-19); Mungu alilinde taifa letu la Tanzania, pamoja na mataifa mengine. Mungu awaponye wagonjwa walio mahospitalini, na awafariji wote waliofiwa kutokana na  ugonjwa huu. Amina.

MWANAUME KWENYE NAFASI YA "MUME"

Mume ni mwanaume aliyeoa kwa kuzingatia vigezo na taratibu za kijamii, kishria na za kiroho. Mume si rafiki wa kiume (boyfriend), hawara, wa...

Powered By Blogger