Thursday, 17 November 2016

JE, KUNA TOFAUTI GANI KATI YA ‘CASFETA’ NA ‘CASFETA (TAYOMI)’?


Bwana Yesu Asifiwe!
Napenda kukualika katika kulitazama swali hili ambalo najua baadhi ya watu hawapendi kabisa kulisikia kwa sababu linahusu swala ambalo liliwajeruhi sana watumishi wa Mungu. Nimelileta swali hili kwa sababu ya changamoto kubwa niliyoiona na ninayoendelea kuiona kwa kizazi hiki. Katika kipindi hiki ambapo elimu imepewa kipaumbele sana, watoto wetu wanatumia muda mwingi sana mashuleni. Hivyo, kama hapatakuwa na usimamizi wa kueleweka tutawaweka katika wakati mgumu sana.

Kwanza, napenda kumshukuru sana Mungu kwa kuwepo kwa makundi haya ambayo yamefayika msaada mkubwa sana kwa maisha ya watu wengi waliopata nafasi ya kupita katika mfumo wa elimu hapa nchini kwetu. Wapo wengi walioanza maisha ya wokovu kutokana na utendaji wa makundi haya (nikiwepo mimi mwenyewe) na wengine wengi wameweza kusimama katika huduma zao na wokovu kwa ujumla kwa sababu ya kulelewa katika makundi haya.

Pili, nieleze sasa lililomo moyoni mwangu, wapendwa, “Ni muda mrefu sana nimekuwa nikishuhudia changamoto wanazokutana nazo wanafunzi wa Kipentekoste mashuleni hasa wa vikundi hivi viwili vyenye jina moja la ‘CASFETA’. Sijui kama wewe msomaji wangu kama ulishashuhudia changamoto yoyote katika makundi haya?

Naamini kama hujashuhudia inawezekana umesikia kwa mwanao au viongozi wa makanisa au hata kwa watu maeneo mbalimbali.”  Kuna maeneo mengine wanafunzi hawapatani na baadhi ya wachungaji, wengine wanagombana wao kwa wao, yaani ni vurugu tupu. Kila mmoja anateta jina la kikundi chake. Wakati natafakari hili nikakumbuka Paulo alivyosema,

“…kwa maana hata sasa ninyi ni watu wa tabia ya mwilini. Maana, ikiwa kwenu kuna husuda na fitina, je! Si watu wa tabia ya mwilini ninyi; tena mnaenenda kwa jinsi ya kibinadamu? Maana hapo mtu mmoja asemapo, Mimi ni wa Paulo; na mwingine, Mimi ni wa Apolo, je! Ninyi si wanadamu? Basi Apolo ni nani? Na Paulo ni nani? Ni wahudumu ambao kwao mliamini; na kila mtu kama Bwana alivyompa. Mimi nilipanda, Apolo akatia maji; bali mwenye kukuza ni Mungu. Hivyo, apandaye si kitu, wala atiaye maji, bali Mungu akuzaye.”

Bado nikawa ninawaza, kuna nini kinachowafanya hawa watoto wetu wasipatane na wakamtumikia Mungu kwa pamoja kwa amani. Nimepata baadhi ya mambo ya kihistoria lakini bado ninaamini huu ni wakati wetu wa kulitazama jambo hili kwa upya. Kizazi kijacho kinatuhitaji sana ili kiweze kusimamia yote yaliyowekwa mbele yake kuyafanya.

Baada ya  kulitazama swala hili kwa kina, ndipo nikabaki na swali kubwa moyoni mwangu juu ya utofauti uliopo kati ya makundi haya mawili yenye jina moja. Kwa nini swali hili likanijia na kunisumbua? Nitakueleza mambo kadhaa niliyoyatafakari ili nawe uyatafakari, niayangu sio kukosoa vikundi hivi ila ni kukutazamisha hali ambayo inaweza kuwakosesha wengi mbingu kama hatutaishughulikia mapema. 

JINA LA MAKUNDI HAYA
Kinachonishangaza hapa ni kwamba makundi haya yanayojihesabu kuwa makundi mawili yenye lengo la kuwalea wanafunzi wa Kipentekoste wawapo masomoni yanaitwa kwa jina moja yaani CASFETA (Christ’s Ambassadors Students’ Fellowship of Tanzania). Sasa inakuwaje makundi tofauti yakaitwa kwa jina moja? Najua majibu yapo kutokana na historia ya makundi haya, ila nakuuliza ili uweze kutafakari kwa upana zaidi. Je, ilikuwaje jina moja likasimamia maono ya aina mbili tofauti?


       2.  MAONO NA UTENDAJIKAZI
Katika uzoefu wangu wa miaka zaidi ya 10 masomoni yakiwepo yale ya Kidato cha kwanza hadi cha nne (O-Level), ya kidato cha tano na sita (A-Level) pamoja nay ale ya Chuo kikuu miaka mitatu (UDSM) nimekuwa nikijifunza sana mambo mengi katika makundi yote mawili. Mwisho nikagundua kwamba haya makundi yana maono yanayofanana na yanafanya kazi katika msingi mmoja huku wakitumia mbinu zinazofanana katika usiamamizi na uendeshaji wa ibada.

       3. WASHIRIKI WA KILA KUNDI
Kila kundi linadai kwamba linafanya kazi na wanafunzi wa makanisa yote ya Kipentekoste yaani EAGT, TAG, FPCT, KLPT, PENTEKOSTE PEFA, PENTEKOSTE HOLINESS NA MENGINE MENGI, kwa kifupi ni yale makanisa ambayo yapo kwenye umoja wa makanisa ya Kipentekoste (PCT). Kwa hiyo mshiriki ni lazima awe amebatizwa kwa maji tele, na awe anaabudu katika moja ya makanisa ya Kipentekoste. Kwa hiyo katika makundi yote mawili utakuta mchanganyiko wa wanafunzi wa madhehebu mbalimbali ya Kipentekoste.

         4. MSIMAMO WA KIIMANI
Kama nilivyosema kwenye swala la washiriki kwamba wote ni wa Imani ya Kipentekoste, yaani wanasimamia misingi ya Kipentekoste wakisistiza hasa ile yenye utata kwa baadhi ya watu mfano Ujazo wa Roho Mtakatifu na kunena kwa lugha mpya, Ubatizo wa maji tele na ule wa kuukiri wokovu wazi wazi. Viongozi na washiriki wote katika makundi haya ni lazima asimamie misingi hii kuhakikisha inakuwa hai kwenye maisha yao ya kila siku yaani, wajazwe nguvu za Roho Mtakatifu, wanene kwa lugha mpya na ni lazima wawe wamebatizwa kwa maji tele kama maandiko yasemavyo.

      5.  MISISTIZO YA MSINGI (Mambo ya muhimu)
Makundi yote mawili yameweka msisitizo mkubwa kwenye swala Utakatifu, Neno la Mungu, Maombi, Utumishi wa mtu mmoja mmoja na wa kikundi kama viungo katika mwili wa Kristo, Mafanikio ya kimasomo kama sehemu ya kumtangaza Kristo, Malezi ya kiroho makanisani (Kila mshiriki ni lazima awe na kanisa linalomlea kiroho), Utoaji wa kibiblia (Hasa Fungu la 10) na mengine.

Baada ya kuyaangalia mambo haya pamoja na mimi japo kwa ufupi naamini na wewe umeanza kujiuliza swali nilililojiuliza, “Kwani kuna tofauti gani?” Je, unayo majibu ya Swali hili? Kama unazo hebu zipime na kuziangalia tena mara mbili mara tatu.

Hebu nikushirikishe changamoto chache nilizoziona kwa kuwepo kwa makundi haya mawili yenye jina moja.
                 i.          Migogoro kati ya viongozi
Nimeshuhudia migogoro ya maneno na ile ya kimya kimya kati ya viongozi wengi wa makundi haya, hasa kwa yale yanayofanya kazi kwenye taasisi moja (Shule au Chuo). Migogoro hii imekuwa ikiibuka hasa kwenye maeneo mbalimbali likiwemo eneo la washiriki ambapo baadhi ya viongozi wamekuwa wakinyang’anyana washiriki na wengine kujitahidi kuwajengea washiriki wake maneno mabaya kuhusu kundi la pili ili wahame (kuwalinda). Kila kundi linajitahidi kuonyesha utofauti wake ambao kiuhalisia hauonekani au hauna nguvu kubwa.
               ii.          Kutangatanga kwa vijana waliookoka mashuleni na vyuoni
Kwa sababu wengi huwa hawaoni tofauti kati ya makundi haya mawili, wengi huwa na uhuru wa kwenda kundi lolote kati ya haya mawili. Mwingine utakuta ameshiriki kwenye makundi haya kwa nyakati tofautitofauti kutokana na anavyoona mwenyewe.
              iii.          Mwonekano kwa wasiomjua Mungu na waongofu wapya
Wengi huwa katika maswali mengi wakijiuliza juu ya tofauti iliyopo kati ya makundi haya, wakati mwingine viongozi wa makundi hutumia muda mwingi kuwaelimisha juu ya utofauti huo ili kuweza kuwajengea msimamo badala ya kuwalea katika misingi ya kibiblia.
              iv.          Walezi na wadau mbalimbali wa Injili kwa wanafunzi na vijana
Changamoto hii hutokea pale ambapo utakuta mtumishi wa Mungu amepata maono ya kuwafikia wanafunzi wa kipentekoste kwa umoja wao. Hapa ni lazima aulizwe unawatafuta wa CASFETA ipi? Na hili huleta ugumu pia katika kuwaunganisha na kuwaleta pamoja.
               v.          Changamoto kwenye uanzishwaji wa matawi mashuleni
Tumeshuhudia migongano mingi kwenye hili eneo, ambapo utakuta CASFETA iliyotangulia inajitahidi kuipiga vita inayoingia ili isiwavuruge washiriki wake. Japo kwenye baadhi ya maeneo kuna makubaliano yanayofanyika bado hakupo kutazamana vizuri kwa makundi haya.
Katika kutafakari nikasema, “Sasa ni nini sababu ya utofauti huu? Au ni nini Tatizo?
Baadhi ya watu wakasema “tatizo ni waanzilishi wake”, nami nikasema “kwani hawa waanzilishi sio Wapentekoste? Hawajatoka kwenye makanisa haya ya kipentekoste?” nikagundua kwamba wote ni wapentekoste wazuri.

      Wengine wakasema “labda ni Madhehebu wanayotoka hao washiriki”, hapa napo nikajiuliza “kwani makundi haya hayana watu kutoka madhehebu mbali mbali?” (Nikagundua wala hakuna ubaguzi wa kidhehebu kwenye makundi haya)

Wengine wakasema tofauti inatokana na walezi wa makundi haya: yaani CASFETA inalelewa na Kanisa la TAG (Tanzania Assemblies of God) na CASFETA (TAYOMI) inalelewa na Tanzania Youth Ministries (TAYOMI). Kwa upande wangu nikajiuliza kuna tofauti gani ya malezi kati ya walezi hawa? Je, Wanafunzi hawa si wa makanisa yote ya Kipentekoste? Japo baadhi ya makanisa nayo yameshaanzisha vyombo vyao. Je, hii roho ya kuwabagua watoto huku tukiwaita jina moja ilitoka wapi? Je, wokovu wetu si mmoja (imani moja, ubatizo mmoja, Roho mmoja) au kuna nini kimefichika?

     Wengine wakasema ni matunda ya ule mgogoro uliokuwepo kati TAG na EAGT kwenye miaka ya 1980 na 90, bado hapa nikajiuliza kwa hiyo ile roho ya matengano hakufa bado? Ni kweli kwamba ndiyo inayoendelea kukitafuna hata kizazi hiki ambacho hakina hatia (Hakikuwepo wakati wa mgogoro)? Bado sikuweza kukubaliana nao asilimia mia moja.

    Hebu sasa nikuulize na wewe mpendwa, ikiwa ni mchungaji, Askofu, mwimbaji, kiongozi wa CASFETA mstaafu, Mwana-CASFETA, mshirika wa kanisa la Kipentekoste na mdau mwingine yeyote unayejishughulisha na malezi ya wanafunzi mashuleni. Je, Kuna tofauti gani kati ya CASFETA na CASFETA (TAYOMI)? 

Mimi ninawalilia watoto wanaopigana vita isiyowahusu. Au niseme, "baba za watu wamekula zabibu kali, na meno ya watoto wao yametiwa ganzi." Matengano haya yanawatesa watoto wetu. Chuki ya CASFETA na CASFETA (TAYOMI) haina Mungu ndani yake. Sumu hii ni lazima itafutiwe dawa, ili kuokoa maisha ya vijana mashuleni. Wachungaji wengi wanawapiga vita wanafunzi kwa sababu ya chuki kati ya makundi haya mawili. Kanisa la Kristo Yesu liko wapi katika mashindano na malumbano. 

Hakunatofauti kati ya CASFETA na CASFETA (TAYOMI), ni lazima watoto wetu wajue Kristo hajagawanyika. Wote ni wa Kristo, Kristo ni mmoja. Tutumike katika upendo, na wazazi wa kiroho (Maaskofu na Wachungaji) msaidie kusimamia jambo hili. Huduma nyingi zinazimwa kwa sababu ya mitazamo hasi iliyojengeka katika makundi haya.

"Eee Mungu likumbuke kanisa la Tanzania, Wakumbuke wanafunzi wetu mashuleni, na wasaidie viongozi wetu walione kusudi lako kwa watoto na vijana walio mashuleni."

Na Mwl. S.S.Michael
Simu: 0713511544 (Whatsapp)
AGM - International.


Wednesday, 16 November 2016

USISHINDANE NA MUNGU

YA NINI KUSHINDANA NA MUNGU?
Isaya 45:9 “Ole wake ashindanaye na Muumba wake! Kigae kimoja katika vigae vya dunia! Je! Udongo umwambie yeye aufinyangaye; Unafanya nini? Au kazi yako, Hana mikono?”
Kabla ya kumwangalia mwanadamu labda nikukumbushe kwamba Shetani (Lucifer) ndiye aliyekuwa wa kwanza kuinua kiburi na kushindana na  Mungu. Kumbuka alikuwa Isaya 14:13 Nawe ulisema moyoni mwako, Nitapanda mpaka mbinguni, Nitakiinua kiti changu juu kuliko nyota za Mungu; Nami nitaketi juu ya mlima wa mkutano, Katika pande za mwisho za kaskazini.” Hiki ni kiburi cha hali ya juu sana, ndiyo maana Mungu akakasirika akamtupa chini kuzimu na kumhukumu milele. 
Shetani yeye kwa sababu alikuwa Kerubi wa sifa kwa Mungu, tunaweza kusema hizo sifa ndizo zlizompa kiburi hata akashindana na Mungu. Je, wewe mwanadamu wa leo ni nini kinakupa kiburi? Je, ni mali! Kumbuka nchi na vyote viijazavyo ni mali ya Mungu. Je, ni uwezo ulionao kitaaluma? Kumbuka Mungu ndiye aliyekuumba na kukupa huo uwezo. Je, ni sura (urembo)! Kumbuka sisi sote ni mavumbi.
Ukisoma biblia utagundua kwamba mwanadamu amekuwa katika hali ya kutaka kushindana na Mungu hasa kwa sababu Mungu haonekani kwa macho ya damu na nyama. Tangu Adamu na Eva walipofanya uasi katika bustani ya Edeni, hali ya uasi iliendelea kukaa katika moyo wa mwanadamu hata kufikia mahali pa kupata kiburi na kutaka kushindana na Mungu.
Katika Mwanzo 6:3, Bwana (Mungu) akasema, Roho yangu haitashindana na mwanadamu milele, kwa kuwa yeye naye ni nyama; basi siku zake zitakuwa miaka mia na ishirini.
Ukisoma kuanzia mstari wa kwanza utaona kwamba wanadamu waliongezeka sana, na wakazidi kufanya maasi mengi hata kuvuruga kabisa ile mipaka ambayo Mungu amewawekea. Mstari wa 5 unasema “Bwana akaona ya kuwa maovu ya mwanadamu ni makubwa duniani na kwamba kila kusudi analowaza moyoni mwake ni baya tu sikuzote.”
Mashindano haya hayakuisha, yamekuwa yakiendelea hata katika kizazi hiki.
Tunashindana na Mungu kwa njia gani?
  1. Kuukosoa uumbaji wake.
Kusudi la Mungu ni kila kitu kiende kwa utaratibu aliouweka kulingana na kusudi lake. Ila katika kizazi cha leo kuna watu ambao wamekuwa wagumu wa kuelewa na wamekuwa wakipindua mambo. Mtume Paulo akisema na warumi aliwazungumzia watu wa jinsi hii.
Warumi 1:26 – 27 “Hivyo Mungu aliwaacha wafuate tamaa zao za aibu, hata wanawake wakabadili matumizi ya asili kwa matumizi yasiyo ya asili; wanaume nao vivyo hivyo waliyaacha matumizi ya mke, ya asili, wakawakiana tamaa, wanaume wakiyatenda yasiyopasa, wakapata nafsini mwao malipo ya upotevu wao yaliyo haki yao.” Unaona mapinduzi haya? Huku ni kushindana na Mungu.
Hapa anazungumzia maswala ya “Ushoga”  ndoa za jinsia moja na kufanya mapenzi kinyume na maumbile. Huku ni kwenda kinyume na utaratibu wa Mungu na kwa lugha rahisi ni kushindana na Mungu. Matokeo yake ni magumu sana. Hapo juu tuliposoma panatuweka wazi kwamba “Kuna kuachwa na Mungu” na hii ndiyo sababu ya ugumu wa maisha duniani.
2.  Kwa kupingana na neno  lake.
Wako watu wengi siku hizi wanaojaribu kulipindua neno la Mungu na kuleta mafundisho yao kulingana na matakwa yao. Hii ni kushindana na Mungu. Lile neno alilolisema Mungu ni AMINI na KWELI, sisi kazi yetu ni kutii tu. Tukimchukua Farao kama mfano tunaweza kuona ni jinsi gani Mungu anavyoweza kulisimamia neno lake. Mungu anamwambia “WAPE WATU WAANGU RUHUSA WAENDE WAKANITUMIKIE” (Kutoka 5:1, 8:1)
Ona majibu ya Farao Kutoka 5:2 “Farao akasema, Bwana ni nani, hata niisikilize sauti yake, na kuwapa Israeli ruhusa waende zao? Mimi simjui Bwana, wala sitawapa Israeli ruhusa waende zao.” Hiki ni kiburi cha hali ya juu sana, na ni hali ambayo inaweza kuonekana kwa watu wengi wenye madaraka au utajiri. Wako watu wenye mioyo kama Farao, hawako tayari kulitii neno la Mungu. Huku ni kushindana na Mungu!
3. Kwa kutenda dhambi (Uasi)
Katika 1Yohana 3:4 tunasoma, Kila atendaye dhambi, afanya uasi; kwa kuwa dhambi ni uasi.” Kwa hiyo kutenda dhambi mbali na kumtenga mtu na Mungu, huinua pia roho ya mtu kuwa na kiburi na wakati mwingine hata kumsema Mungu vibaya.
Roho ya kuasi ni roho mbaya sana, katika mwanzo 6 tumeona maovu wa wanadamu yaliongezeka sana na Mungu akatangaza wazi kwamba Roho yake haitashindana na mwanadamu.
4. Kupigana au kuwapiga vita watumishi wake.
 Hili ni jambo ambalo watu katika nyakati za leo wameliona la kawaida tu. Kumbe sio jambo la kawaida, uscheze na mpakwa mafuta wa Mungu.
Mfalme Daudi alijua swala na Mashihi wa Bwana kabla hata ya kuwa Mfalme. 1 Samweli 26:9 “Lakini Daudi akamwambia Abishai, Usimwangamize; kwani ni nani awezaye kuunyosha mkono wake juu ya masihi”
Ukisoma tena, Zaburi 20:6 Daudi anaimba Zaburi na kusema “Sasa najua kuwa Bwana amwokoa masihi wake;Atamjibu kutoka mbingu zake takatifu.” Nakatika  Zaburi 28:8 anasema “Bwana ni nguvu za watu wake, Naye ni ngome ya wokovu kwa masihi wake.”
Tunachijifunza hasa kwenye mistari hii ya Zaburi ni kwamba, unaposhindana na masihi au mpakwa mafuta wa Bwana unashindana naye (Mungu) mwenyewe. Tunaliona pale Miriamu alipojaribu kumsema vibaya Musa mtumishi wa Mungu. (Hesabu 12) Mungu alimpa adhabu kali sana, hakutaka kusikia hata maombi ya Musa na Haruni. Miriamu alipata Ukoma na alifungwa  nje ya kambi kwa muda wa siku saba.
Tukumbuke pia wakati wa akina Daniel kule Babeli vile ambavyo Mungu alishughulika na watu walioshindana na watumishi wake. Kipindi cha Akina Petro Mungu alimshughulikia. Matendo 12:22 “Watu wakapiga kelele, wakisema, Ni sauti ya Mungu, si sauti ya mwanadamu. Mara malaika wa Bwana akampiga, kwa sababu hakumpa Mungu utukufu; akaliwa na chango, akatokwa na roho.”
Ni muhimu pia tukamkumbuka Paulo wakati anajulikana kama Sauli,aliyekuwa mkatili, akuia watu waliokuwa wanamtaja Yesu na kuamini. Ukiso Matendo 9 utaona taarifa za Sauli. Mstari wa kwanza tunasoma, “Lakini Sauli, akizidi kutisha na kuwaza kuwaua wanafunzi wa Bwana”
Aliua wengi lakini mwisho akakutana na Mungu akamshikisha adabu, Mstari wa 8 na 9 tunasoma, “ Sauli akainuka katika nchi, na macho yake yalipofumbuka, hakuona kitu; wakamshika mkono wakamleta mpaka Dameski. Akawa siku tatu haoni; hali, wala hanywi.
5. Kuabudu miungu (Kumfananisha Mungu na vitu au watu)
Katika Warumi 1: 21-23 “kwa sababu, walipomjua Mungu hawakumtukuza kama ndiye Mungu wala kumshukuru; bali walipotea katika uzushi wao, na mioyo yao yenye ujinga ikatiwa giza.Wakijinena kuwa wenye hekima walipumbazika; wakaubadili utukufu wa Mungu asiye na uharibifu kwa mfano wa sura ya binadamu aliye na uharibifu, na ya ndege, na ya wanyama, na ya vitambaavyo.”
Kumbuka pia wakati Musa amekwenda mlimai akawaacha Wana wa Israeli Jangwani wakiongozwa na Haruni; kisha Haruni akawatengenezea Sanamu ya ndama ili waiabudu, Mungu alighadhibika sana akataka kuwaangamiza wote.
Kutoka 32, ukisoma huu mlango utaona madhara makubwa yaliyotokea kwa sababu ya jambo hili.
Waamuzi 2:12 Tunausoma wakati ambapo Israeli nao walimwacha Mungu wakaabudu sanamu, “Wakamwacha Bwana, Mungu wa baba zao, aliyewaleta kutoka katika nchi ya Misri, wakafuata miungu mingine, baadhi ya miungu ya watu wale waliokaa karibu nao pande zote, wakajiinamisha mbele yao; wakamkasirisha Bwana, akaghadhibika. Napo matokeo yake hayakuwa mazuri, mambo yaliwaharibikia kabisa.
6.  Maneno ya Kiburi na kuingilia kazi za madhabahu.
Jinsi nyingine ya kushindana na Mungu ni kwa kuzungumza maneno ya kiburi, na kujiinua juu ya Mungu.  Maneno kama haya yalimgharimu Herode, alipoongea watu wakamsifu basi ikawa ndio mwisho wake.
Mfalme Uzia naye alifanya vizuri sana mbele za Mungu, kisha akawa na kiburi akaenda akaingilia kazi ya makuhani; kazi ya kuvukiza uvumba madhabahuni pa Bwana. Hata alipoelekezwa na makuhani hakutaka kusikia kabisa. Alijiona mwenye haki mahali ambapo Mungu hakumweka. Lililomtokea mwenyewe alishika adabu.
2Nyakati 26:19-21 “ ukamtokea ukoma katika paji la uso wake mbele ya makuhani nyumbani mwa Bwana karibu na madhabahu ya kufukizia na …. angalia, alikuwa na ukoma pajini mwa uso, wakamtoa humo upesi; hata na yeye mwenyewe akafanya haraka kutoka, kwa sababu Bwana amempiga. Uzia mfalme akawa na ukoma hata siku ya kufa kwake, akakaa katika nyumba ya pekee, kwa kuwa ni mwenye ukoma; maana alitengwa na nyumba ya Bwana”
          Katika dunia hii tuna watu wengi sana ambao wamejaa maneno ya kiburi, wengine ni kwa sababu ya nafasi zao za uongozi, wengine ni utajiri, wengine ni umaarufu, wengine ni sura na vile walivyo kwa nje. Watu hawa wanashindana na Mungu bila kujua nap engine kwa kujua. Ni muhimu tukajifunza kwa hawa waliojaribu kuongea maneno ya kiburi Mungu akashughulika nao.
Nirudie tena swali langu la Msingi “U nani wewe unayeshindana na Mungu?” Katika mstari wetu wa msingi tumesoma, Ole wake ashindanaye na Muumba wake! Kigae kimoja katika vigae vya dunia! Je! Udongo umwambie yeye aufinyangaye; Unafanya nini? Au kazi yako, Hana mikono?”
Unapojaribu kushindana na Mungu kumbuka mambo haya:
  1.       Hakuna aliyewahi kushindana na Mungu akashinda
  2.     Sisi sote kwa jinsi ya mwili ni mavumbi,tuliumbwa kwa mavumbi na huko tutarudi (mwanzo 3:16)
  3.      Uko hivyo ulivyo kwa neema ya Mungu tu Nchi na vyote viijazavyo ni mali ya Mungu
  4.        Ukigusa utukufu wa Mungu huwezi kuendele kuishi
  5.     Tulikuja uchi na bila kitu na hatutaondoka na kitu. 1 Timotheo 6:7 “Kwa maana hatukuja na kitu duniani, tena hatuwezi kutoka na kitu”


JE, UNAISHI KULINGANA NA KUSUDI LA MUNGU JUU YA MAISHA YAKO?

TAFUTA KUTIMIZA KUSUDI LA MUNGU
KATIKA KILA UNALOLIFANYA.

Utangulizi:

Kila jambo litakalokujia wewe kama mtumishi wa Mungu jua kwamba lina muunganiko na kusudi unalolitumikia kwa wakati huo au unaloelekea kulitumikia. Jambo lolote liwe baya au jema, liwe gumu au jepesi, uwe unalijua au haulijui, liwe la kawaida au lisiwe la kawaida.

Nafasi au fursa zote anazofungua au alizofungua Mungu kwako , vita anavyoleta shetani, hali ya mwili wako binafsi-usumbufu, umbo, sura nk; hali ya kiuchumi, familia uliyotoka, maeneo uliyopita na yote uliyofanya katika maisha uliyoishi ni lazima yawe na matokeo ya namna moja au nyingine katika kusudi unalotumikia au utakalotumikia.
🔃🔃
Kila mahali Mungu anapokupeleka ni lazima pawe na kusudi lake, wakati mwingie kusudi lake ni kukuandaa kwaajili ya kusudi jingine. Kila unalofanya likikufanya utimize kusudi la Mungu  rahisi kuona mafanikio makubwa yakiandamana nawe kila wakati.

Muhubiri 3:1-8
Kwa kila jambo kuna majira yake, Na WAKATI kwa kila kusudi chini ya mbingu. WAKATI wa kuzaliwa, na WAKATI wa kufa; WAKATI wa kupanda, na WAKATI wa kung'oa yaliyopandwa; WAKATI wa kuua, na WAKATI wa kupoza; WAKATI wa kubomoa, na WAKATI wa kujenga; WAKATI wa kulia, na WAKATI wa kucheka; WAKATI wa kuomboleza, na WAKATI wa kucheza; WAKATI wa kutupa mawe, na WAKATI wa kukusanya mawe; WAKATI wa kukumbatia, na WAKATI wa kutokumbatia; WAKATI wa kutafuta, na WAKATI wa kupoteza; WAKATI wa kuweka, na WAKATI wa kutupa; WAKATI wa kurarua, na WAKATI wa kushona; WAKATI wa kunyamaza, na WAKATI wa kunena; WAKATI wa kupenda, na WAKATI wa kuchukia; WAKATI WA VITA, NA WAKATI WA AMANI.

MSINGI WA SOMO
1Tim. 4:8 -10
Kwa maana kujizoeza kupata nguvu za mwili kwafaa kidogo, lakini utauwa hufaa kwa mambo yote; yaani, unayo ahadi ya uzima wa sasa, na ya ule utakaokuwapo baadaye. Ni neno la kuaminiwa, tena lastahili kukubalika kabisa; kwa maana twajitaabisha na kujitahidi KWA KUSUDI HILI, kwa sababu tunamtumaini Mungu aliye hai, aliye Mwokozi wa watu wote, hasa wa waaminio.
Wafilipi 2:13
Kwa maana ndiye Mungu atendaye kazi ndani yenu, kutaka kwenu na kutenda kwenu, kwa kulitimiza kusudi lake jema.
Yeremia 29:11-14
Maana nayajua MAWAZO NINAYOWAWAZIA ninyi, asema Bwana, ni mawazo ya amani wala si ya mabaya, kuwapa ninyi tumaini siku zenu za mwisho.NANYI MTANIITA, mtakwenda na KUNIOMBA, nami NITAWASIKILIZA. NANYI MTANITAFUTA na KUNIONA, mtakaponitafuta KWA MOYO wenu wote. NAMI NITAONEKANA KWENU, asema Bwana, NAMI NITAWARUDISHA watu wenu waliofungwa, nami nitawakusanya ninyi, nikiwatoa katika mataifa yote, na katika mahali pote, nilikowafukuza, asema Bwana; nami nitawaleta tena, hata mahali ambapo kutoka hapo naliwafanya mchukuliwe mateka.

MAMBO MATATU
*     Yajue mawazo ya Mungu juu ya kusudi unalolitumikia au unalojiandaa kulitumikia. (Mawazo Mungu anayokuwazia)
-       1kor. 2:12 Lakini sisi hatukuipokea roho ya dunia, bali Roho atokaye kwa Mungu, MAKUSUDI tupate kuyajua tuliyokirimiwa na Mungu.
-       Zaburi 92:5 Ee Bwana, jinsi yalivyo makuu matendo yako! Mawazo yako ni mafumbo makubwa.
-       Mika 4:12 Lakini wao hawayajui mawazo ya Bwana, wala hawafahamu shauri lake; kwa maana amewakusanya kama miganda sakafuni.
-       Zaburi 139:17-18 Mungu, fikira zako zina thamani nyingi kwangu; Jinsi livyo kubwa jumla yake! Kama ningezihesabu ni nyingi kuliko mchanga; Niamkapo nikali pamoja nawe.
*     Hakikisha unamuona Mungu kabla hujaondoka kupiga hatua/ wewe binafsi uhakikishwe katika hilo unaloliendea.
-       Kutoka 33:15 Naye akamwambia, Uso wako usipokwenda pamoja nami, usituchukue kutoka hapa.
-       Mathayo 12:30 Mtu asiye pamoja nami yu kinyume changu; na mtu asiyekusanya pamoja nami hutapanya.
-       KUTOKA 3:7 – 14
Bwana akasema, Hakika nimeyaona mateso ya watu wangu walioko Misri, nami nimekisikia kilio chao kwa sababu ya wasimamizi wao; maana nayajua maumivu yao; nami nimeshuka ili niwaokoe na mikono ya Wamisri, niwapandishe kutoka nchi ile, hata nchi njema, kisha pana; nchi ijaayo maziwa na asali; hata mahali pa Mkanaani, na Mhiti, na Mwamori, na Mperizi, na Mhivi, na Myebusi. Basi, tazama, kilio cha wana wa Israeli kimenifikilia; tena nimeyaona hayo mateso ambayo Wamisri wanawatesa. Haya, basi, nitakutuma sasa kwa Farao, ili upate kuwatoa watu wangu, hao wana wa Israeli, katika Misri. Musa akamwambia Mungu, Mimi ni nani, hata niende kwa Farao, nikawatoe wana wa Israeli watoke Misri? Akasema, Bila shaka mimi nitakuwa pamoja nawe; na dalili ya kuwa nimekutuma ndiyo hii; utakapokuwa umekwisha kuwatoa hao watu katika Misri, mtamwabudu Mungu katika mlima huu. Musa akamwambia Mungu, Tazama, nitakapofika kwa wana wa Israeli, na kuwaambia, Mungu wa baba zenu amenituma kwenu; nao wakaniuliza, Jina lake n'nani? Niwaambie nini? Mungu akamwambia Musa, MIMI NIKO AMBAYE NIKO;akasema,Ndivyo utakavyowaambia wana wa Israeli; MIMI NIKO amenituma kwenu.

-       Mdo. 9: 3-16
Hata alipokuwa akisafiri, ikawa anakaribia Dameski; ghafula ikamwangaza kote kote nuru kutoka mbinguni. Akaanguka chini, akasikia sauti ikimwambia, Sauli, Sauli, mbona waniudhi? Akasema, U nani wewe, Bwana? Naye akasema, Mimi ndimi Yesu unayeniudhi wewe. Lakini simama, uingie mjini, nawe utaambiwa yakupasayo kutenda. ……………… Basi palikuwapo Dameski mwanafunzi jina lake Anania. Bwana akamwambia katika maono, Anania.
Akasema, Mimi hapa, Bwana. Bwana akamwambia, Simama, enenda zako katika njia iitwayo Nyofu, ukaulize katika nyumba ya Yuda mtu aitwaye Sauli, wa Tarso; maana, angalia, anaomba; naye amemwona mtu, jina lake Anania, akiingia, na kumwekea mikono juu yake, apate kuona tena.
Lakini Anania akajibu, Bwana, nimesikia habari za mtu huyu kwa watu wengi, mabaya mengi aliyowatenda watakatifu wako Yerusalemu; hata hapa ana amri itokayo kwa wakuu wa makuhani awafunge wote wakuitiao Jina lako. Lakini Bwana akamwambia, Nenda tu; kwa maana huyu ni chombo kiteule kwangu, alichukue Jina langu mbele ya Mataifa, na wafalme, na wana wa Israeli. Maana nitamwonyesha yalivyo mengi yatakayompasa kuteswa kwa ajili ya Jina langu.

*     Mwandalie Mungu mazingira ya kuonekana unapoendelea. –“nami nitaonekana kwenu...”
-       Mfanyie Mungu nafasi katika kutimiza kwako hayo ambayo una uhakika ni makusudi ya Mungu.
-       Ambatana na madhabahu ya Mungu
-       Mungu aone nafasi yake katika kufanikiwa kwako.
-       Tunza Ibada

Ili Mungu aonekane kwenye jambo lolote ni lazima aione heshima yake kwanza, na apewe nafasi ya kuweza kuonekana. Mwanadamu peke yake ndiye mwenye nafasi ya kumfanya Mungu ajidhihirishe katika eneo lolote. 

Tuesday, 15 November 2016

JE, NI NINI HUTOKEA MARA TU MTU ANAPOOKOKA?

YAPO MENGI HUTOKEA.
“Hata imekuwa, mtu akiwa ndani ya Kristo amekuwa kiumbe kipya; ya kale yamepita tazama! Yamekuwa mapya” 2 Wakorintho 5:17
Ni vema mtu unapoamua kuokoka ukatambua mabadiliko ya msingi ambayo hutoe pao kwa papo ambayo, yanakufanya kuwa mtu wa tofauti na ulivyokuwa mwanzoni. Mtu anapokubali kuokoka, hutokea mabadiliko katika maeneo makuu manne.
A.     Mbinguni (Kwenye Ufalme wa Mungu).
Katika kitabu cha Luka15:10 Nawaambia, Vivyo hivyo kuna furaha mbele ya malaika wa Mungu kwa ajili ya mwenye dhambi mmoja atubuye” Kwa hiyo kunakuwa na furaha mbinguni juu ya kurejea kwako katika Ufalme wa Mungu (ulikuwa mwana aliyepotea)  Neno linasema “malaika wa mbinguni anafurahia” mtu anapoamua kutubu na kumrudia Mungu.
Jambo jingine ambalo hutokea mbinguni ni, jina kuandikwa katika kitabu cha uzima. Luka 10:20 “Lakini, msifurahi kwa vile pepo wanavyowatii; bali furahini kwa sababu majina yenu yameandikwa mbinguni.” Wanafunzi walipokuwa wanafurahia utendaji kazi wa nguvu za Mungu; Yesu anawakumbusha kwamba jambo la kufurahia zaidi ni kule majina yao kuandikwa mbinguni na sio mapepo kutii. Kumbuka Yesu alikuja ili aturejeshe kwa Mungu, na majina yetu yatambulike tena mbinguni.
Ufunuo 21:27 “Na ndani yake hakitaingia kamwe cho chote kilicho kinyonge, wala yeye afanyaye machukizo na uongo, bali wale walioandikwa katika kitabu cha uzima cha Mwana-Kondoo. Hapa tunaona wenye fursa ya kuingia mbinguni ni wale tu ambao majina yao yameandikwa kwenye Kitabu cha uzima.
Wafilipi 4:3 “…. na wale wengine waliotenda kazi pamoja nami, ambao majina yao yamo katika kitabu cha uzima.” Mtume Paulo anaongea kwa uhakika kabisa akijua ya kwamba mtu anapoamua kuokoka moja kwa moja jina lake linaandikwa katika kitabu cha Uzima.
Revelation 20:15 “Na iwapo mtu ye yote hakuonekana ameandikwa katika kitabu cha uzima, alitupwa katika lile ziwa la moto.” Hapa tunaona adhabu ya mtu ambaye jina lake halitaonekana kwenye kitabu cha uzima, kwamba atatupwa kwenye ziwa la moto (Jehanamu). Jambo hili linatupa kujipeleleza na kuona kama majina yetu kweli yameandikwa mbinguni.
Je, utajuaje jina langu limeandikwa mbinguni? Ni rahisi tu kujua, kama umetubu kweli na kumkiri Yesu kuwa Bwana na mwokozi wa maisha yako na kusimama katika utakatifu basi jina lako litakuwepo kwenye kitabu cha Uzima. Hiki ni kitabu cha watakatifu, yaani wale waliokubali kusafishwa kwa Damu ya Yesu kama tulivyoona kwamba Yesu alijisafishia watu ili wawe milki yake. Tena Roho Mtakatifu wa Mungu atakushuhudi ndani yako.
Tatu, unapata kibali cha kupokea siri na Baraka za rohoni ndani yake Kristo. Mtu anapokuwa hajaokoka anakuwa amefungwa na katika utu wa kale ambao hauna ushirika na Mungu. Hivyo anakuwa hana uwezo wa kurithi Baraka pamoja na Yesu. 1Korintho14 Basi mwanadamu wa tabia ya asili hayapokei mambo ya Roho wa Mungu; maana kwake huyo ni upuzi, wala hawezi kuyafahamu, kwa kuwa yatambulikana kwa jinsi ya rohoni.
Kwa hiyo kwa kumpokea Yesu kuwa Bwana na Mwokozi wetu, tumefungua mlango wa kupokea kipawa cha Roho Mtakatifu na kupokea nguvu na karama mbalimbali kutoka kwa Mungu.
Nne, Kumbukumbu za matendo yako mabaya zinafutwa, na kuanza ukurasa mpya wa maisha. Maandiko yanatuthibitishia kwamba hakuna dhambi inayokumbukwa tena, baada ya kutubu kweli na kumwamini Yesu. Katika Isaya 1:18
“Mungu anasema, Haya, njoni, tusemezane, asema Bwana. Dhambi zenu zijapokuwa nyekundu Sana, zitakuwa nyeupe Kama theluji; zijapokuwa nyekundu Kama bendera, zitakuwa kama sufu”.
Isaya 43: 25 “Mimi, naam, mimi, ndimi niyafutaye makosa yako kwa ajili yangu mwenyewe, wala sitazikumbuka dhambi zako.”
1Yohana 1:9 “Tukiziungama dhambi zetu, Yeye ni mwaminifu na wa haki hata atuondolee dhambi zetu, na kutusafisha na udhalimu wote.”
Kwa hiyo katika maneno haya tunapata ujasiri wa moja kwa moja kwamba mtu anapokubali kutubu dhambi na kuziacha kisha kumwishia Kristo katika maisha yake yote, maovu na dhambi zote alizozitenda vinafutwa kabisa. Tena, Mungu anasema hatazikumbuka tena na hakutakuwa na hukumu tna juu yake.
Tano, Uhusiano wako na Mungu unarejea upya; Kumbuka Yesu alikuja kufanya upatanisho kati ya mwanadamu mwenye dhambi na Mungu Mtakatifu. 2 Wakorintho 5:19 yaani, Mungu alikuwa ndani ya Kristo, akiupatanisha ulimwengu na nafsi yake, asiwahesabie makosa yao; naye ametia ndani yetu neno la upatanisho.
B.     Kwenye mazingira yake (Duniani)
Unakuwa wakili wa Mungu katika dunia hii. Katika 1 Wakorintho 4:1 Paulo anasema, “Mtu na atuhesabu hivi, kuwa tu watumishi wa Kristo, na mawakili wa siri za Mungu.” Tena Mtume Petro anasema, “Kila mmoja kwa kadiri alivyoipokea karama, itumieni kwa kuhudumiana; kama mawakili wema wa neema mbalimbali za Mungu” 1 Petro 4:10. Kwa hiyo ni lazima ujijue kwamba Mungu anataka akutumie kama mwakilishi wake hapa duniani katika eneo alilokuweka.
Unarejeshewa mamlaka ya kutawala na kumiliki pamoja na Kristo Yesu, Ufunuo 5:9-10 “Nao waimba wimbo mpya wakisema, Wastahili wewe kukitwaa hicho kitabu na kuzifungua muhuri zake; kwa kuwa ulichinjwa, ukamnunulia Mungu kwa damu yako watu wa kila kabila na lugha na jamaa na taifa,ukawafanya kuwa ufalme na makuhani kwa Mungu wetu; nao wanamiliki juu ya nchi.”Kwa hiyo, tunapokuwa ndani ya Kristo tunakuwa tumerejeshewa ile mamlaka tuliyoipoteza kupitia dhambi ya Adamu katika bustani ya Edeni.
Unakuwa adui wa dunia/unatengwa na dunia. 1Yohana 2:15 “Msiipende dunia, wala mambo yaliyomo katika dunia. Mtu akiipenda dunia, kumpenda Baba hakumo ndani yake. Maana kila kilichomo duniani, yaani, tamaa ya mwili, na tamaa ya macho, na kiburi cha uzima, havitokani na Baba, bali vyatokana na dunia. Na dunia inapita, pamoja na tamaa zake, bali yeye afanyaye mapenzi ya Mungu adumu hata milele.”
Warumi 8:7Kwa kuwa ile nia ya mwili ni uadui juu ya Mungu, kwa maana haitii sheria ya Mungu, wala haiwezi kuiti.”
Yakobo 4:4Enyi wazinzi, hamjui ya kwamba kuwa rafiki wa dunia ni kuwa adui wa Mungu? Basi kila atakaye kuwa rafiki wa dunia hujifanya kuwa adui wa Mungu.”Kumbe Mungu anatutaka tukajitenge na uovu wa kila namna na kuuvaa utakatifu pamoja na Kristo.

C.     Kwenye maisha binafsi
Unakuwa kiumbe kipya. 2 Wakorintho 5:17Hata imekuwa, mtu akiwa ndani ya Kristo amekuwa kiumbe kipya; ya kale yamepita tazama! Yamekuwa mapya.”Hapa tunaelezwa wazi kabisa kwamba ndani ya Yesu tunakuwa viumbe vipya, tena yale mambo ya kale (ya dunia) yamepita.
Unafanyika mtoto/mwana wa Mungu. Yohana 1:12 “Bali wote waliompokea aliwapa uwezo wa kufanyika watoto wa Mungu, ndio wale waliaminio jina lake.” Warumi 8:16Roho mwenyewe hushuhudia pamoja na roho zetu, ya kuwa sisi tu watoto wa Mungu.” Ni muhimu sana ukajua kuwa sasa wewe ni mtoto wa Mungu, na Mungu ni Baba yako.
Unapata raha nafsini baada ya kuondolewa mizigo na kusamehewa dhambi. Mathayo 11:29 “Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu Tena katika Warumi 6:22 Mtume Paulo anazungumza juu ya kuwekwa huru mbali na dhambi, “Lakini sasa mkiisha kuwekwa huru, na kuwa mbali na dhambi, na kufanywa watumwa wa Mungu, mnayo faida yenu, ndiyo kutakaswa, na mwisho wake ni uzima wa milele.”
Neema ya kuwekwa huru kutoka kwenye vifungo inakuwa juu yako. Wakolosai 1:13 Naye alituokoa katika nguvu za giza, akatuhamisha na kutuingiza katika ufalme wa Mwana wa pendo lake; ambaye katika yeye tuna ukombozi, yaani, msamaha wa dhambi” Unapokuwa ndani ya Kristo shetani anakuwa hana tena mamlaka ya kukaa ndani yako, hivyo unakuwa huru mbali na aina zote za vifungo. Japo maombi huwa yanahitajika ili mtu aweze kuwekwa huru kabisa. Yakobo anatupa kanuni moja ya msingi sana katika maisha yetu ya wokovu; anasema, “Basi mtiini Mungu. Mpingeni Shetani, naye atawakimbia.” Yakobo 4:7
Mfumo wa kufikiria na kuamua unabadilika. Wakolosai 3:2 Yafikirini yaliyo juu, siyo yaliyo katika nchi. Tena Paulo katika Warumi 12:2-3 anatupa ushauri wa msingi sana, unaolenga kutusaidia katika kila maamuzi tunayofanya. “Wala msiifuatishe namna ya dunia hii; bali mgeuzwe kwa kufanywa upya nia zenu, mpate kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu. Kwa maana kwa neema niliyopewa namwambia kila mtu aliyeko kwenu asinie makuu kupita ilivyompasa kunia; bali awe na nia ya kiasi, kama Mungu alivyomgawia kila mtu kiasi cha imani.”
Unakuwa mbali na utumwa wa dhambi. Warumi 8:10 “Na Kristo akiwa ndani yenu, mwili wenu umekufa kwa sababu ya dhambi; bali roho yenu i hai, kwa sababu ya haki.”
Yohana 8: 31-32, 34-36 “….Ninyi mkikaa katika neno langu, mmekuwa wanafunzi wangu kweli kweli; tena mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru. Yesu akawajibu, Amin, amin, nawaambia, Kila atendaye dhambi ni mtumwa wa dhambi. Wala mtumwa hakai nyumbani sikuzote; mwana hukaa sikuzote. Basi Mwana akiwaweka huru, mtakuwa huru kweli kweli.”
Mistari hii inatuonyesha kwamba tulikuwa watumwa wa dhambi lakini sasa YESU anatuweka huru kabisa.
Unapokea vipawa na karama, pamoja na nguvu za Roho Mtakatifu. Matendo ya Mitume 2:38 “Petro akawaambia, Tubuni mkabatizwe kila mmoja kwa jina lake Yesu Kristo, mpate ondoleo la dhambi zenu, nanyi mtapokea kipawa cha Roho Mtakatifu.” Tena kwenye Waefeso 4:8 Paulo anasema, “Hivyo husema, Alipopaa juu aliteka mateka, Akawapa wanadamu vipawa.”
Unaanza mfumo mpya wa mahusiano. Waefeso 2:14 Kwa maana yeye ndiye amani yetu, aliyetufanya sisi sote tuliokuwa wawili kuwa mmoja; akakibomoa kiambaza cha kati kilichotutenga.” Hapa tunaona kulikuwa na matengano katikati ya wanadamu, ila Yesu alipokuja akajenga mahusiano upya. Katika Mathayo tano Yesu anatoa kanuni mpya za mahusiano.
Mathayo 5:38-45 “Mmesikia kwamba imenenwa, Jicho kwa jicho, na jino kwa jino; Lakini mimi nawaambia, Msishindane na mtu mwovu; lakini mtu akupigaye shavu la kuume, mgeuzie na la pili. Na mtu atakaye kukushitaki na kuitwaa kanzu yako, mwachie na joho pia. Na mtu atakayekulazimisha mwendo wa maili moja, nenda naye mbili. Akuombaye, mpe; naye atakaye kukopa kwako, usimpe kisogo. Mmesikia kwamba imenenwa, Umpende jirani yako, na, Umchukie adui yako; lakini mimi nawaambia, Wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi, ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni; maana yeye huwaangazia jua lake waovu na wema, huwanyeshea mvua wenye haki na wasio haki.”
Mfumo wa uchumi na kazi unabadilika. Mathayo 6:33-34 “Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa. Basi msisumbukie ya kesho; kwa kuwa kesho itajisumbukia yenyewe. Yatosha kwa siku maovu yake. Mathayo 12:30 Mtu asiye pamoja nami yu kinyume changu; na mtu asiyekusanya pamoja nami hutapanya. Kwa hiyo baada ya kuokoka Ufalme wa Mungu unakuwa mbele, na tunakusanya pamoja na Mungu.
Tabia za Mungu zinaanza kudhihirika ndani yako kwa msaada wa Roho mtakatifu, na tabia za kidunia zinakosa nguvu. Wagalatia 5:22 “Lakini tunda la Roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi; juu ya mambo kama hayo hakuna sheria.”
D.    Kuzimu (Kwenye ufalme wa Shetani)
Jina linafutwa kwenye kumbukumbu za shetani. Wakolosai 1:13 Naye alituokoa katika nguvu za giza, akatuhamisha na kutuingiza katika ufalme wa Mwana wa pendo lake. Kuwa katika nguvu za giza maana yake tulikuwa katika himaya ya shetani, kumbukumbu zetu zilionekana kwa shetani. Tunapookoka kibao kinageuka, mambo yote yanafutwa.
Hati ya mashitaka inafutwa.  Katika Wakolosai 2:14 Paulo anasema, “akiisha kuifuta ile hati iliyoandikwa ya kutushitaki kwa hukumu zake, iliyokuwa na uadui kwetu; akaiondoa isiwepo tena, akaigongomea msalabani”.
Shetani anatangaza mpango rasmi wa kukutafuta.  1 Petro 5:8 Mwe na kiasi na kukesha; kwa kuwa mshitaki wenu Ibilisi, kama simba angurumaye, huzunguka-zunguka, akitafuta mtu ammeze. Kwa hiyo ni muhimu ukatambua kwamba, kuzimu kuna mpango maalumu umekwisha kuwekwa ili kuhakikisha kwamba unarudi tena mikononi mwa shetani. Ni wewe sasa kusimama vizuri na Yesu anayesema, Wote anipao Baba watakuja kwangu; wala ye yote ajaye kwangu sitamtupa nje kamwe. Yohana 6:37
Kimsingi, Mambo haya yanatuonyesha kuwa kuna mabadiliko makubwa ambayo hutokea mara tu matu anapoamua kuokoka (Kumpa Yesu Kristo maisha yake) Mabadiliko haya ndiyo humfanya mtu aone uhalisia wa wokovu katika maisha yake, na kumpa ujasiri wa kusimama katika upya kila siku. Tunaambiwa kwamba Neema YA Mungu hutufundisha kuukataa ubaya na tama za kidunia kisha tunapata kuishi kwa kiasi, na haki na utauwa katika ulimwengu huu wa sasa. Haya ni mabadiliko makubwa sana.
Katika Mathayo  3:8 “Yohana akawaambia Wayahudi, “Basi zaeni matunda yapasayo toba” Tena Paulo anawaambia Wafilipi “Lakini mwenendo wenu na uwe kama inavyoipasa Injili ya Kristo” (Wafilipi 1:27)
Tena kwenye Waefeso 4:22 anasema, “mvue kwa habari ya mwenendo wa kwanza utu wa zamani, unaoharibika kwa kuzifuata tamaa zenye kudanganya”
2Wakorintho 5:17 inasema, “Hata imekuwa, mtu akiwa ndani ya Kristo amekuwa kiumbe kipya; ya kale yamepita tazama! Yamekuwa mapya.

Mistari hii inathibitisha zaidi na kukazia swala la kuwa na badiliko kamili na lenye matunda yaliyokusudiwa kwa majira na nyakati. Yaani matunda yaipasayo Toba na matunda yaipasayo Injili.

MWANAUME KWENYE NAFASI YA "MUME"

Mume ni mwanaume aliyeoa kwa kuzingatia vigezo na taratibu za kijamii, kishria na za kiroho. Mume si rafiki wa kiume (boyfriend), hawara, wa...

Powered By Blogger