Tuesday, 15 November 2016

JE, NI NINI HUTOKEA MARA TU MTU ANAPOOKOKA?

YAPO MENGI HUTOKEA.
“Hata imekuwa, mtu akiwa ndani ya Kristo amekuwa kiumbe kipya; ya kale yamepita tazama! Yamekuwa mapya” 2 Wakorintho 5:17
Ni vema mtu unapoamua kuokoka ukatambua mabadiliko ya msingi ambayo hutoe pao kwa papo ambayo, yanakufanya kuwa mtu wa tofauti na ulivyokuwa mwanzoni. Mtu anapokubali kuokoka, hutokea mabadiliko katika maeneo makuu manne.
A.     Mbinguni (Kwenye Ufalme wa Mungu).
Katika kitabu cha Luka15:10 Nawaambia, Vivyo hivyo kuna furaha mbele ya malaika wa Mungu kwa ajili ya mwenye dhambi mmoja atubuye” Kwa hiyo kunakuwa na furaha mbinguni juu ya kurejea kwako katika Ufalme wa Mungu (ulikuwa mwana aliyepotea)  Neno linasema “malaika wa mbinguni anafurahia” mtu anapoamua kutubu na kumrudia Mungu.
Jambo jingine ambalo hutokea mbinguni ni, jina kuandikwa katika kitabu cha uzima. Luka 10:20 “Lakini, msifurahi kwa vile pepo wanavyowatii; bali furahini kwa sababu majina yenu yameandikwa mbinguni.” Wanafunzi walipokuwa wanafurahia utendaji kazi wa nguvu za Mungu; Yesu anawakumbusha kwamba jambo la kufurahia zaidi ni kule majina yao kuandikwa mbinguni na sio mapepo kutii. Kumbuka Yesu alikuja ili aturejeshe kwa Mungu, na majina yetu yatambulike tena mbinguni.
Ufunuo 21:27 “Na ndani yake hakitaingia kamwe cho chote kilicho kinyonge, wala yeye afanyaye machukizo na uongo, bali wale walioandikwa katika kitabu cha uzima cha Mwana-Kondoo. Hapa tunaona wenye fursa ya kuingia mbinguni ni wale tu ambao majina yao yameandikwa kwenye Kitabu cha uzima.
Wafilipi 4:3 “…. na wale wengine waliotenda kazi pamoja nami, ambao majina yao yamo katika kitabu cha uzima.” Mtume Paulo anaongea kwa uhakika kabisa akijua ya kwamba mtu anapoamua kuokoka moja kwa moja jina lake linaandikwa katika kitabu cha Uzima.
Revelation 20:15 “Na iwapo mtu ye yote hakuonekana ameandikwa katika kitabu cha uzima, alitupwa katika lile ziwa la moto.” Hapa tunaona adhabu ya mtu ambaye jina lake halitaonekana kwenye kitabu cha uzima, kwamba atatupwa kwenye ziwa la moto (Jehanamu). Jambo hili linatupa kujipeleleza na kuona kama majina yetu kweli yameandikwa mbinguni.
Je, utajuaje jina langu limeandikwa mbinguni? Ni rahisi tu kujua, kama umetubu kweli na kumkiri Yesu kuwa Bwana na mwokozi wa maisha yako na kusimama katika utakatifu basi jina lako litakuwepo kwenye kitabu cha Uzima. Hiki ni kitabu cha watakatifu, yaani wale waliokubali kusafishwa kwa Damu ya Yesu kama tulivyoona kwamba Yesu alijisafishia watu ili wawe milki yake. Tena Roho Mtakatifu wa Mungu atakushuhudi ndani yako.
Tatu, unapata kibali cha kupokea siri na Baraka za rohoni ndani yake Kristo. Mtu anapokuwa hajaokoka anakuwa amefungwa na katika utu wa kale ambao hauna ushirika na Mungu. Hivyo anakuwa hana uwezo wa kurithi Baraka pamoja na Yesu. 1Korintho14 Basi mwanadamu wa tabia ya asili hayapokei mambo ya Roho wa Mungu; maana kwake huyo ni upuzi, wala hawezi kuyafahamu, kwa kuwa yatambulikana kwa jinsi ya rohoni.
Kwa hiyo kwa kumpokea Yesu kuwa Bwana na Mwokozi wetu, tumefungua mlango wa kupokea kipawa cha Roho Mtakatifu na kupokea nguvu na karama mbalimbali kutoka kwa Mungu.
Nne, Kumbukumbu za matendo yako mabaya zinafutwa, na kuanza ukurasa mpya wa maisha. Maandiko yanatuthibitishia kwamba hakuna dhambi inayokumbukwa tena, baada ya kutubu kweli na kumwamini Yesu. Katika Isaya 1:18
“Mungu anasema, Haya, njoni, tusemezane, asema Bwana. Dhambi zenu zijapokuwa nyekundu Sana, zitakuwa nyeupe Kama theluji; zijapokuwa nyekundu Kama bendera, zitakuwa kama sufu”.
Isaya 43: 25 “Mimi, naam, mimi, ndimi niyafutaye makosa yako kwa ajili yangu mwenyewe, wala sitazikumbuka dhambi zako.”
1Yohana 1:9 “Tukiziungama dhambi zetu, Yeye ni mwaminifu na wa haki hata atuondolee dhambi zetu, na kutusafisha na udhalimu wote.”
Kwa hiyo katika maneno haya tunapata ujasiri wa moja kwa moja kwamba mtu anapokubali kutubu dhambi na kuziacha kisha kumwishia Kristo katika maisha yake yote, maovu na dhambi zote alizozitenda vinafutwa kabisa. Tena, Mungu anasema hatazikumbuka tena na hakutakuwa na hukumu tna juu yake.
Tano, Uhusiano wako na Mungu unarejea upya; Kumbuka Yesu alikuja kufanya upatanisho kati ya mwanadamu mwenye dhambi na Mungu Mtakatifu. 2 Wakorintho 5:19 yaani, Mungu alikuwa ndani ya Kristo, akiupatanisha ulimwengu na nafsi yake, asiwahesabie makosa yao; naye ametia ndani yetu neno la upatanisho.
B.     Kwenye mazingira yake (Duniani)
Unakuwa wakili wa Mungu katika dunia hii. Katika 1 Wakorintho 4:1 Paulo anasema, “Mtu na atuhesabu hivi, kuwa tu watumishi wa Kristo, na mawakili wa siri za Mungu.” Tena Mtume Petro anasema, “Kila mmoja kwa kadiri alivyoipokea karama, itumieni kwa kuhudumiana; kama mawakili wema wa neema mbalimbali za Mungu” 1 Petro 4:10. Kwa hiyo ni lazima ujijue kwamba Mungu anataka akutumie kama mwakilishi wake hapa duniani katika eneo alilokuweka.
Unarejeshewa mamlaka ya kutawala na kumiliki pamoja na Kristo Yesu, Ufunuo 5:9-10 “Nao waimba wimbo mpya wakisema, Wastahili wewe kukitwaa hicho kitabu na kuzifungua muhuri zake; kwa kuwa ulichinjwa, ukamnunulia Mungu kwa damu yako watu wa kila kabila na lugha na jamaa na taifa,ukawafanya kuwa ufalme na makuhani kwa Mungu wetu; nao wanamiliki juu ya nchi.”Kwa hiyo, tunapokuwa ndani ya Kristo tunakuwa tumerejeshewa ile mamlaka tuliyoipoteza kupitia dhambi ya Adamu katika bustani ya Edeni.
Unakuwa adui wa dunia/unatengwa na dunia. 1Yohana 2:15 “Msiipende dunia, wala mambo yaliyomo katika dunia. Mtu akiipenda dunia, kumpenda Baba hakumo ndani yake. Maana kila kilichomo duniani, yaani, tamaa ya mwili, na tamaa ya macho, na kiburi cha uzima, havitokani na Baba, bali vyatokana na dunia. Na dunia inapita, pamoja na tamaa zake, bali yeye afanyaye mapenzi ya Mungu adumu hata milele.”
Warumi 8:7Kwa kuwa ile nia ya mwili ni uadui juu ya Mungu, kwa maana haitii sheria ya Mungu, wala haiwezi kuiti.”
Yakobo 4:4Enyi wazinzi, hamjui ya kwamba kuwa rafiki wa dunia ni kuwa adui wa Mungu? Basi kila atakaye kuwa rafiki wa dunia hujifanya kuwa adui wa Mungu.”Kumbe Mungu anatutaka tukajitenge na uovu wa kila namna na kuuvaa utakatifu pamoja na Kristo.

C.     Kwenye maisha binafsi
Unakuwa kiumbe kipya. 2 Wakorintho 5:17Hata imekuwa, mtu akiwa ndani ya Kristo amekuwa kiumbe kipya; ya kale yamepita tazama! Yamekuwa mapya.”Hapa tunaelezwa wazi kabisa kwamba ndani ya Yesu tunakuwa viumbe vipya, tena yale mambo ya kale (ya dunia) yamepita.
Unafanyika mtoto/mwana wa Mungu. Yohana 1:12 “Bali wote waliompokea aliwapa uwezo wa kufanyika watoto wa Mungu, ndio wale waliaminio jina lake.” Warumi 8:16Roho mwenyewe hushuhudia pamoja na roho zetu, ya kuwa sisi tu watoto wa Mungu.” Ni muhimu sana ukajua kuwa sasa wewe ni mtoto wa Mungu, na Mungu ni Baba yako.
Unapata raha nafsini baada ya kuondolewa mizigo na kusamehewa dhambi. Mathayo 11:29 “Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu Tena katika Warumi 6:22 Mtume Paulo anazungumza juu ya kuwekwa huru mbali na dhambi, “Lakini sasa mkiisha kuwekwa huru, na kuwa mbali na dhambi, na kufanywa watumwa wa Mungu, mnayo faida yenu, ndiyo kutakaswa, na mwisho wake ni uzima wa milele.”
Neema ya kuwekwa huru kutoka kwenye vifungo inakuwa juu yako. Wakolosai 1:13 Naye alituokoa katika nguvu za giza, akatuhamisha na kutuingiza katika ufalme wa Mwana wa pendo lake; ambaye katika yeye tuna ukombozi, yaani, msamaha wa dhambi” Unapokuwa ndani ya Kristo shetani anakuwa hana tena mamlaka ya kukaa ndani yako, hivyo unakuwa huru mbali na aina zote za vifungo. Japo maombi huwa yanahitajika ili mtu aweze kuwekwa huru kabisa. Yakobo anatupa kanuni moja ya msingi sana katika maisha yetu ya wokovu; anasema, “Basi mtiini Mungu. Mpingeni Shetani, naye atawakimbia.” Yakobo 4:7
Mfumo wa kufikiria na kuamua unabadilika. Wakolosai 3:2 Yafikirini yaliyo juu, siyo yaliyo katika nchi. Tena Paulo katika Warumi 12:2-3 anatupa ushauri wa msingi sana, unaolenga kutusaidia katika kila maamuzi tunayofanya. “Wala msiifuatishe namna ya dunia hii; bali mgeuzwe kwa kufanywa upya nia zenu, mpate kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu. Kwa maana kwa neema niliyopewa namwambia kila mtu aliyeko kwenu asinie makuu kupita ilivyompasa kunia; bali awe na nia ya kiasi, kama Mungu alivyomgawia kila mtu kiasi cha imani.”
Unakuwa mbali na utumwa wa dhambi. Warumi 8:10 “Na Kristo akiwa ndani yenu, mwili wenu umekufa kwa sababu ya dhambi; bali roho yenu i hai, kwa sababu ya haki.”
Yohana 8: 31-32, 34-36 “….Ninyi mkikaa katika neno langu, mmekuwa wanafunzi wangu kweli kweli; tena mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru. Yesu akawajibu, Amin, amin, nawaambia, Kila atendaye dhambi ni mtumwa wa dhambi. Wala mtumwa hakai nyumbani sikuzote; mwana hukaa sikuzote. Basi Mwana akiwaweka huru, mtakuwa huru kweli kweli.”
Mistari hii inatuonyesha kwamba tulikuwa watumwa wa dhambi lakini sasa YESU anatuweka huru kabisa.
Unapokea vipawa na karama, pamoja na nguvu za Roho Mtakatifu. Matendo ya Mitume 2:38 “Petro akawaambia, Tubuni mkabatizwe kila mmoja kwa jina lake Yesu Kristo, mpate ondoleo la dhambi zenu, nanyi mtapokea kipawa cha Roho Mtakatifu.” Tena kwenye Waefeso 4:8 Paulo anasema, “Hivyo husema, Alipopaa juu aliteka mateka, Akawapa wanadamu vipawa.”
Unaanza mfumo mpya wa mahusiano. Waefeso 2:14 Kwa maana yeye ndiye amani yetu, aliyetufanya sisi sote tuliokuwa wawili kuwa mmoja; akakibomoa kiambaza cha kati kilichotutenga.” Hapa tunaona kulikuwa na matengano katikati ya wanadamu, ila Yesu alipokuja akajenga mahusiano upya. Katika Mathayo tano Yesu anatoa kanuni mpya za mahusiano.
Mathayo 5:38-45 “Mmesikia kwamba imenenwa, Jicho kwa jicho, na jino kwa jino; Lakini mimi nawaambia, Msishindane na mtu mwovu; lakini mtu akupigaye shavu la kuume, mgeuzie na la pili. Na mtu atakaye kukushitaki na kuitwaa kanzu yako, mwachie na joho pia. Na mtu atakayekulazimisha mwendo wa maili moja, nenda naye mbili. Akuombaye, mpe; naye atakaye kukopa kwako, usimpe kisogo. Mmesikia kwamba imenenwa, Umpende jirani yako, na, Umchukie adui yako; lakini mimi nawaambia, Wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi, ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni; maana yeye huwaangazia jua lake waovu na wema, huwanyeshea mvua wenye haki na wasio haki.”
Mfumo wa uchumi na kazi unabadilika. Mathayo 6:33-34 “Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa. Basi msisumbukie ya kesho; kwa kuwa kesho itajisumbukia yenyewe. Yatosha kwa siku maovu yake. Mathayo 12:30 Mtu asiye pamoja nami yu kinyume changu; na mtu asiyekusanya pamoja nami hutapanya. Kwa hiyo baada ya kuokoka Ufalme wa Mungu unakuwa mbele, na tunakusanya pamoja na Mungu.
Tabia za Mungu zinaanza kudhihirika ndani yako kwa msaada wa Roho mtakatifu, na tabia za kidunia zinakosa nguvu. Wagalatia 5:22 “Lakini tunda la Roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi; juu ya mambo kama hayo hakuna sheria.”
D.    Kuzimu (Kwenye ufalme wa Shetani)
Jina linafutwa kwenye kumbukumbu za shetani. Wakolosai 1:13 Naye alituokoa katika nguvu za giza, akatuhamisha na kutuingiza katika ufalme wa Mwana wa pendo lake. Kuwa katika nguvu za giza maana yake tulikuwa katika himaya ya shetani, kumbukumbu zetu zilionekana kwa shetani. Tunapookoka kibao kinageuka, mambo yote yanafutwa.
Hati ya mashitaka inafutwa.  Katika Wakolosai 2:14 Paulo anasema, “akiisha kuifuta ile hati iliyoandikwa ya kutushitaki kwa hukumu zake, iliyokuwa na uadui kwetu; akaiondoa isiwepo tena, akaigongomea msalabani”.
Shetani anatangaza mpango rasmi wa kukutafuta.  1 Petro 5:8 Mwe na kiasi na kukesha; kwa kuwa mshitaki wenu Ibilisi, kama simba angurumaye, huzunguka-zunguka, akitafuta mtu ammeze. Kwa hiyo ni muhimu ukatambua kwamba, kuzimu kuna mpango maalumu umekwisha kuwekwa ili kuhakikisha kwamba unarudi tena mikononi mwa shetani. Ni wewe sasa kusimama vizuri na Yesu anayesema, Wote anipao Baba watakuja kwangu; wala ye yote ajaye kwangu sitamtupa nje kamwe. Yohana 6:37
Kimsingi, Mambo haya yanatuonyesha kuwa kuna mabadiliko makubwa ambayo hutokea mara tu matu anapoamua kuokoka (Kumpa Yesu Kristo maisha yake) Mabadiliko haya ndiyo humfanya mtu aone uhalisia wa wokovu katika maisha yake, na kumpa ujasiri wa kusimama katika upya kila siku. Tunaambiwa kwamba Neema YA Mungu hutufundisha kuukataa ubaya na tama za kidunia kisha tunapata kuishi kwa kiasi, na haki na utauwa katika ulimwengu huu wa sasa. Haya ni mabadiliko makubwa sana.
Katika Mathayo  3:8 “Yohana akawaambia Wayahudi, “Basi zaeni matunda yapasayo toba” Tena Paulo anawaambia Wafilipi “Lakini mwenendo wenu na uwe kama inavyoipasa Injili ya Kristo” (Wafilipi 1:27)
Tena kwenye Waefeso 4:22 anasema, “mvue kwa habari ya mwenendo wa kwanza utu wa zamani, unaoharibika kwa kuzifuata tamaa zenye kudanganya”
2Wakorintho 5:17 inasema, “Hata imekuwa, mtu akiwa ndani ya Kristo amekuwa kiumbe kipya; ya kale yamepita tazama! Yamekuwa mapya.

Mistari hii inathibitisha zaidi na kukazia swala la kuwa na badiliko kamili na lenye matunda yaliyokusudiwa kwa majira na nyakati. Yaani matunda yaipasayo Toba na matunda yaipasayo Injili.

No comments:

Post a Comment

MWANAUME KWENYE NAFASI YA "MUME"

Mume ni mwanaume aliyeoa kwa kuzingatia vigezo na taratibu za kijamii, kishria na za kiroho. Mume si rafiki wa kiume (boyfriend), hawara, wa...

Powered By Blogger