Wednesday, 16 November 2016

USISHINDANE NA MUNGU

YA NINI KUSHINDANA NA MUNGU?
Isaya 45:9 “Ole wake ashindanaye na Muumba wake! Kigae kimoja katika vigae vya dunia! Je! Udongo umwambie yeye aufinyangaye; Unafanya nini? Au kazi yako, Hana mikono?”
Kabla ya kumwangalia mwanadamu labda nikukumbushe kwamba Shetani (Lucifer) ndiye aliyekuwa wa kwanza kuinua kiburi na kushindana na  Mungu. Kumbuka alikuwa Isaya 14:13 Nawe ulisema moyoni mwako, Nitapanda mpaka mbinguni, Nitakiinua kiti changu juu kuliko nyota za Mungu; Nami nitaketi juu ya mlima wa mkutano, Katika pande za mwisho za kaskazini.” Hiki ni kiburi cha hali ya juu sana, ndiyo maana Mungu akakasirika akamtupa chini kuzimu na kumhukumu milele. 
Shetani yeye kwa sababu alikuwa Kerubi wa sifa kwa Mungu, tunaweza kusema hizo sifa ndizo zlizompa kiburi hata akashindana na Mungu. Je, wewe mwanadamu wa leo ni nini kinakupa kiburi? Je, ni mali! Kumbuka nchi na vyote viijazavyo ni mali ya Mungu. Je, ni uwezo ulionao kitaaluma? Kumbuka Mungu ndiye aliyekuumba na kukupa huo uwezo. Je, ni sura (urembo)! Kumbuka sisi sote ni mavumbi.
Ukisoma biblia utagundua kwamba mwanadamu amekuwa katika hali ya kutaka kushindana na Mungu hasa kwa sababu Mungu haonekani kwa macho ya damu na nyama. Tangu Adamu na Eva walipofanya uasi katika bustani ya Edeni, hali ya uasi iliendelea kukaa katika moyo wa mwanadamu hata kufikia mahali pa kupata kiburi na kutaka kushindana na Mungu.
Katika Mwanzo 6:3, Bwana (Mungu) akasema, Roho yangu haitashindana na mwanadamu milele, kwa kuwa yeye naye ni nyama; basi siku zake zitakuwa miaka mia na ishirini.
Ukisoma kuanzia mstari wa kwanza utaona kwamba wanadamu waliongezeka sana, na wakazidi kufanya maasi mengi hata kuvuruga kabisa ile mipaka ambayo Mungu amewawekea. Mstari wa 5 unasema “Bwana akaona ya kuwa maovu ya mwanadamu ni makubwa duniani na kwamba kila kusudi analowaza moyoni mwake ni baya tu sikuzote.”
Mashindano haya hayakuisha, yamekuwa yakiendelea hata katika kizazi hiki.
Tunashindana na Mungu kwa njia gani?
  1. Kuukosoa uumbaji wake.
Kusudi la Mungu ni kila kitu kiende kwa utaratibu aliouweka kulingana na kusudi lake. Ila katika kizazi cha leo kuna watu ambao wamekuwa wagumu wa kuelewa na wamekuwa wakipindua mambo. Mtume Paulo akisema na warumi aliwazungumzia watu wa jinsi hii.
Warumi 1:26 – 27 “Hivyo Mungu aliwaacha wafuate tamaa zao za aibu, hata wanawake wakabadili matumizi ya asili kwa matumizi yasiyo ya asili; wanaume nao vivyo hivyo waliyaacha matumizi ya mke, ya asili, wakawakiana tamaa, wanaume wakiyatenda yasiyopasa, wakapata nafsini mwao malipo ya upotevu wao yaliyo haki yao.” Unaona mapinduzi haya? Huku ni kushindana na Mungu.
Hapa anazungumzia maswala ya “Ushoga”  ndoa za jinsia moja na kufanya mapenzi kinyume na maumbile. Huku ni kwenda kinyume na utaratibu wa Mungu na kwa lugha rahisi ni kushindana na Mungu. Matokeo yake ni magumu sana. Hapo juu tuliposoma panatuweka wazi kwamba “Kuna kuachwa na Mungu” na hii ndiyo sababu ya ugumu wa maisha duniani.
2.  Kwa kupingana na neno  lake.
Wako watu wengi siku hizi wanaojaribu kulipindua neno la Mungu na kuleta mafundisho yao kulingana na matakwa yao. Hii ni kushindana na Mungu. Lile neno alilolisema Mungu ni AMINI na KWELI, sisi kazi yetu ni kutii tu. Tukimchukua Farao kama mfano tunaweza kuona ni jinsi gani Mungu anavyoweza kulisimamia neno lake. Mungu anamwambia “WAPE WATU WAANGU RUHUSA WAENDE WAKANITUMIKIE” (Kutoka 5:1, 8:1)
Ona majibu ya Farao Kutoka 5:2 “Farao akasema, Bwana ni nani, hata niisikilize sauti yake, na kuwapa Israeli ruhusa waende zao? Mimi simjui Bwana, wala sitawapa Israeli ruhusa waende zao.” Hiki ni kiburi cha hali ya juu sana, na ni hali ambayo inaweza kuonekana kwa watu wengi wenye madaraka au utajiri. Wako watu wenye mioyo kama Farao, hawako tayari kulitii neno la Mungu. Huku ni kushindana na Mungu!
3. Kwa kutenda dhambi (Uasi)
Katika 1Yohana 3:4 tunasoma, Kila atendaye dhambi, afanya uasi; kwa kuwa dhambi ni uasi.” Kwa hiyo kutenda dhambi mbali na kumtenga mtu na Mungu, huinua pia roho ya mtu kuwa na kiburi na wakati mwingine hata kumsema Mungu vibaya.
Roho ya kuasi ni roho mbaya sana, katika mwanzo 6 tumeona maovu wa wanadamu yaliongezeka sana na Mungu akatangaza wazi kwamba Roho yake haitashindana na mwanadamu.
4. Kupigana au kuwapiga vita watumishi wake.
 Hili ni jambo ambalo watu katika nyakati za leo wameliona la kawaida tu. Kumbe sio jambo la kawaida, uscheze na mpakwa mafuta wa Mungu.
Mfalme Daudi alijua swala na Mashihi wa Bwana kabla hata ya kuwa Mfalme. 1 Samweli 26:9 “Lakini Daudi akamwambia Abishai, Usimwangamize; kwani ni nani awezaye kuunyosha mkono wake juu ya masihi”
Ukisoma tena, Zaburi 20:6 Daudi anaimba Zaburi na kusema “Sasa najua kuwa Bwana amwokoa masihi wake;Atamjibu kutoka mbingu zake takatifu.” Nakatika  Zaburi 28:8 anasema “Bwana ni nguvu za watu wake, Naye ni ngome ya wokovu kwa masihi wake.”
Tunachijifunza hasa kwenye mistari hii ya Zaburi ni kwamba, unaposhindana na masihi au mpakwa mafuta wa Bwana unashindana naye (Mungu) mwenyewe. Tunaliona pale Miriamu alipojaribu kumsema vibaya Musa mtumishi wa Mungu. (Hesabu 12) Mungu alimpa adhabu kali sana, hakutaka kusikia hata maombi ya Musa na Haruni. Miriamu alipata Ukoma na alifungwa  nje ya kambi kwa muda wa siku saba.
Tukumbuke pia wakati wa akina Daniel kule Babeli vile ambavyo Mungu alishughulika na watu walioshindana na watumishi wake. Kipindi cha Akina Petro Mungu alimshughulikia. Matendo 12:22 “Watu wakapiga kelele, wakisema, Ni sauti ya Mungu, si sauti ya mwanadamu. Mara malaika wa Bwana akampiga, kwa sababu hakumpa Mungu utukufu; akaliwa na chango, akatokwa na roho.”
Ni muhimu pia tukamkumbuka Paulo wakati anajulikana kama Sauli,aliyekuwa mkatili, akuia watu waliokuwa wanamtaja Yesu na kuamini. Ukiso Matendo 9 utaona taarifa za Sauli. Mstari wa kwanza tunasoma, “Lakini Sauli, akizidi kutisha na kuwaza kuwaua wanafunzi wa Bwana”
Aliua wengi lakini mwisho akakutana na Mungu akamshikisha adabu, Mstari wa 8 na 9 tunasoma, “ Sauli akainuka katika nchi, na macho yake yalipofumbuka, hakuona kitu; wakamshika mkono wakamleta mpaka Dameski. Akawa siku tatu haoni; hali, wala hanywi.
5. Kuabudu miungu (Kumfananisha Mungu na vitu au watu)
Katika Warumi 1: 21-23 “kwa sababu, walipomjua Mungu hawakumtukuza kama ndiye Mungu wala kumshukuru; bali walipotea katika uzushi wao, na mioyo yao yenye ujinga ikatiwa giza.Wakijinena kuwa wenye hekima walipumbazika; wakaubadili utukufu wa Mungu asiye na uharibifu kwa mfano wa sura ya binadamu aliye na uharibifu, na ya ndege, na ya wanyama, na ya vitambaavyo.”
Kumbuka pia wakati Musa amekwenda mlimai akawaacha Wana wa Israeli Jangwani wakiongozwa na Haruni; kisha Haruni akawatengenezea Sanamu ya ndama ili waiabudu, Mungu alighadhibika sana akataka kuwaangamiza wote.
Kutoka 32, ukisoma huu mlango utaona madhara makubwa yaliyotokea kwa sababu ya jambo hili.
Waamuzi 2:12 Tunausoma wakati ambapo Israeli nao walimwacha Mungu wakaabudu sanamu, “Wakamwacha Bwana, Mungu wa baba zao, aliyewaleta kutoka katika nchi ya Misri, wakafuata miungu mingine, baadhi ya miungu ya watu wale waliokaa karibu nao pande zote, wakajiinamisha mbele yao; wakamkasirisha Bwana, akaghadhibika. Napo matokeo yake hayakuwa mazuri, mambo yaliwaharibikia kabisa.
6.  Maneno ya Kiburi na kuingilia kazi za madhabahu.
Jinsi nyingine ya kushindana na Mungu ni kwa kuzungumza maneno ya kiburi, na kujiinua juu ya Mungu.  Maneno kama haya yalimgharimu Herode, alipoongea watu wakamsifu basi ikawa ndio mwisho wake.
Mfalme Uzia naye alifanya vizuri sana mbele za Mungu, kisha akawa na kiburi akaenda akaingilia kazi ya makuhani; kazi ya kuvukiza uvumba madhabahuni pa Bwana. Hata alipoelekezwa na makuhani hakutaka kusikia kabisa. Alijiona mwenye haki mahali ambapo Mungu hakumweka. Lililomtokea mwenyewe alishika adabu.
2Nyakati 26:19-21 “ ukamtokea ukoma katika paji la uso wake mbele ya makuhani nyumbani mwa Bwana karibu na madhabahu ya kufukizia na …. angalia, alikuwa na ukoma pajini mwa uso, wakamtoa humo upesi; hata na yeye mwenyewe akafanya haraka kutoka, kwa sababu Bwana amempiga. Uzia mfalme akawa na ukoma hata siku ya kufa kwake, akakaa katika nyumba ya pekee, kwa kuwa ni mwenye ukoma; maana alitengwa na nyumba ya Bwana”
          Katika dunia hii tuna watu wengi sana ambao wamejaa maneno ya kiburi, wengine ni kwa sababu ya nafasi zao za uongozi, wengine ni utajiri, wengine ni umaarufu, wengine ni sura na vile walivyo kwa nje. Watu hawa wanashindana na Mungu bila kujua nap engine kwa kujua. Ni muhimu tukajifunza kwa hawa waliojaribu kuongea maneno ya kiburi Mungu akashughulika nao.
Nirudie tena swali langu la Msingi “U nani wewe unayeshindana na Mungu?” Katika mstari wetu wa msingi tumesoma, Ole wake ashindanaye na Muumba wake! Kigae kimoja katika vigae vya dunia! Je! Udongo umwambie yeye aufinyangaye; Unafanya nini? Au kazi yako, Hana mikono?”
Unapojaribu kushindana na Mungu kumbuka mambo haya:
  1.       Hakuna aliyewahi kushindana na Mungu akashinda
  2.     Sisi sote kwa jinsi ya mwili ni mavumbi,tuliumbwa kwa mavumbi na huko tutarudi (mwanzo 3:16)
  3.      Uko hivyo ulivyo kwa neema ya Mungu tu Nchi na vyote viijazavyo ni mali ya Mungu
  4.        Ukigusa utukufu wa Mungu huwezi kuendele kuishi
  5.     Tulikuja uchi na bila kitu na hatutaondoka na kitu. 1 Timotheo 6:7 “Kwa maana hatukuja na kitu duniani, tena hatuwezi kutoka na kitu”


No comments:

Post a Comment

MWANAUME KWENYE NAFASI YA "MUME"

Mume ni mwanaume aliyeoa kwa kuzingatia vigezo na taratibu za kijamii, kishria na za kiroho. Mume si rafiki wa kiume (boyfriend), hawara, wa...

Powered By Blogger